Hii Hapa Kauli ya Magesa Mulongo Baada ya Kung'olewa Nafasi ya Ukuu wa Mkoa wa Mara

Rais John Magufuli ametengua uteuzi wa Mkuu wa Mkoa wa Mara, Magesa Mulongo kuanzia jana.


Taarifa iliyotolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Mawasiliano Ikulu, Gerson Msigwa ikimnukuu Katibu Mkuu Kiongozi, Balozi John Kijazi imesema Rais amemteua Dk Charles Mlingwa ambaye alikuwa Mkuu wa Wilaya ya Siha kujaza nafasi hiyo.


Mulongo anakuwa mkuu wa mkoa wa pili kutimuliwa kazi na Rais Magufuli baada ya Anne Kilango Malecela aliyekuwa Shinyanga.


Hata hivyo, tofauti na Kilango ambaye alitimuliwa kutokana na kutoa taarifa potofu kuhusu watumishi hewa mkoani mwake, Ikulu haikutoa sababu za kutenguliwa kwa uteuzi wa Mulongo.


Mulongo ameondolewa madarakani miezi sita baada ya Rais Magufuli kutengua uteuzi wa aliyekuwa Katibu Tawala wa Mkoa wa Mwanza, Dk Faisal Issa baada ya kutofautiana na Mulongo wakati huo akiwa mkuu wa mkoa huo.


Baada ya kumwondoa Dk Issa na nafasi yake kujazwa na aliyekuwa Kamishna wa Polisi, Fedha na Utawala (CP) Clodwig Mtweve, miezi miwili baadaye Rais alimbadilisha Mulongo kituo cha kazi akimhamishia Mara.


Alipoulizwa jana jinsi alivyoipokea hatua hiyo iliyochukuliwa dhidi yake Mulongo alisema: “Sina taarifa rasmi.”

Kabla kuhamishiwa Mara akitokea Mwanza, Mulongo alikuwa Mkuu wa Mkoa wa Arusha.


Alishika nafasi hiyo baada ya kupandishwa cheo akiwa Mkuu wa Wilaya ya Bagamoyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527