Watu 4 Wafariki, 29 Wajeruhiwa Baada ya Basi la HBS Kupinduka Huko Mbeya

Watu wanne wamekufa papo hapo na wengine 29 kujeruhiwa baada ya basi la HBS linalodaiwa kuwa ni mali ya kampuni ya Sabena walilokuwa wakisafiria kutoka jijini Mbeya kwenda Tabora kuacha njia na kupinduka katika eneo la maji mazuri, barabara kuu ya Mbeya – Chunya wilayani Mbeya.

Basi hilo likiwa limebeba abiria wengi kuliko uwezo wake, lilianza safari yake ya kuelekea Tabora likitokea jijini Mbeya, lakini inadaiwa kuwa likiwa kwenye mtelemko na kona kali za mlima Mbeya likafeli breki na ndipo dereva wake akaamua kuruka na kuliacha likijiendesha lenyewe hali ambayo ilisababisha lipoteze mwelekeo na kuanguka mtaroni.


Muuguzi wa zamu katika hospitali ya rufaa ya kanda ya nyanda za juu kusini, Jesca Kahangwa amethibitisha kupokea miili ya watu wanne na majeruhi 29 wa ajali hiyo, huku akidai kuwa hali za majeruhi wengi bado ni mbaya.


Mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama ya mkoa wa Mbeya, Amos Makalla amewahi katika eneo la ajali na baada ya kupata maelezo ya chanzo cha ajali hiyo, akaliagiza jeshi la polisi kuwatafuta na kuwakamata haraka dereva, kondakta na mmiliki wa gari hilo kwa kosa la kuendesha gari bovu barabarani.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527