MKAZI WA SHINYANGA AKAMATWA NA SILAHA NZITO KWENYE BASI LA ABIRIA


Polisi mkoani Morogoro inamshikilia Juma George (29) mkazi wa Shinyanga, kwa kukutwa na silaha ya kivita aina ya SMG iliyofutwa namba zake za usajili, magazini mbili, risasi 21 pamoja na panga vikiwa vimehifadhiwa ndani ya begi lake la nguo.


Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei, alisema mtuhumiwa huyo ambaye ni dereva alikamatwa Machi 30, mwaka huu saa mbili usiku maeneo ya stendi kuu ya mabasi ya Msamvu, mjini Morogoro.


Kamanda Matei alisema, askari wakiwa doria katika eneo hilo walipata taarifa kutoka kwa raia mwema kuwa kwenye basi lenye namba za usajili T.141 DEE aina ya Yutong mali ya Kampuni ya Nyahunge likitokea Shinyanga kwenda Morogoro kuna abiria mmoja amehifadhi silaha.


Alisema baada ya askari kupata taarifa walifika eneo la stendi ya Msamvu na walifanikiwa kumkamata mtu huyo. Ilielezwa kuwa mtuhumiwa huyo alikuwa akitokea mkoani Shinyanga akielekea Tarafa ya Mngeta, wilaya ya Kilombero.


Kamanda wa Polisi Matei alisema, uchunguzi bado unaendelea na utakapokamilika mtuhumiwa atafikishwa mahakamani kujibu shitaka linalomkabili.


Katika tukio jingine, Ester Abel (43) mkazi wa Mbumi B Tarafa ya Kilosa, wilayani Kilosa, mkoani Morogoro anashikiliwa na Polisi kwa kukutwa na dawa za kulevya zinazodhaniwa kuwa ni kokeni kete 780 , kilogramu mbili za bangi na misokoto 25 iliyohifadhiwa kwenye mfuko wa nailoni.


Kamanda wa Polisi wa mkoa wa Morogoro, Matei alisema kuwa mwanamke huyo alikamatwa Machi 30, mwaka huu saa 2:15 usiku katika eneo la Mbumi B , tarafa ya Kilosa Mjini, wilayani humo, mkoani Morogoro .


Kamanda wa Polisi Matei alisema, inadaiwa kuwa mtuhumiwa huyo ni muuzaji wa dawa za kulevya na kwamba uchunguzi unaendelea na atafikishwa mahakamani mara moja baada ya kukamilika kwake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527