MHE. MHAGAMA AAGIZA WAMILIKI WA VYOMBO VYA USAFIRI KUZINGATIA MIKATABA YA KAZI NA AJIRA KWA MADEREVA



Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) akitoa ufafanuzi wa masuala ya mikataba ya ajira wakati wa mkutano na Kamati ya Kudumu ya Waziri Mkuu ya Kutatua kero na changamoto katika sekta ya usafiri wa barabara katika Ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu Aprili 1, 2016.



Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Waziri Mkuu ya Kutatua kero na changamoto katika sekta ya usafiri wa barabara wakifuatilia hoja za Naibu Waziri Uchukuzi Mhe. Edwin Ngonyani (hayupo pichani) wakati wa mkutano wa kamati hiyo April 1,2016 katika Ukumbi wa Ofisi ya Waziri Mkuu.



Mwenyekiti wa Umoja wa Wamiliki wa Daladala Dar es Salaam (DARCOBOA),Sabri Mabrouk akitoa hoja ya uboreshwaji wa mikataba ya madereva wakati wa mkutano wa Kamati ya Kudumu ya Waziri Mkuu ya Kutatua kero na changamoto katika sekta ya usafiri wa barabara uliofanyika  katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu.


Waziri wa Katiba na Sheria Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe akitoa ufafanuzu wa kisheria wakati wa mkutano wa Kamati ya Kudumu ya Waziri Mkuu ya Kutatua kero na changamoto katika sekta ya usafiri wa barabara uliofanyika  katika Ukumbi wa Mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu-(Picha Zote na Ofisi ya Waziri Mkuu)

******

Waziri wa Nchi Ofisi ya Waziri Mkuu (Sera, Bunge, Ajira na Watu wenye Ulemavu) Mhe. Jenista Mhagama (Mb) ameiagiza kamati ya Kudumu ya Waziri Mkuu ya Kutatua kero na changamoto katika sekta ya usafiri wa barabara kuangalia upya mikataba ya madereva ili kuhakikisha haki za madereva zinalindwa.

Mhe mhagama alitoa agizo hilo wakati wa mkutano wake na Kamati hiyo uliofanyika Aprili 1, 2016 katika Ukumbi wa mikutano wa Ofisi ya Waziri Mkuu jijini Dar es Salaam kwa lengo la kuangalia namna bora ya kukabiliana na changamoto zinazoikabili sekta ya usafirishaji.

Katika kikao cha Kamati hiyo inayoundwa na Wamiliki wa malori, daladala, mabasi, vyama vya abiria, Idara ya Usafirishaji, Shirika la viwango, Wakala wa Vipimo, Jeshi la polisi, watu wa usalama barabarani, TANROADS na Umoja wa Wasafirishaji Abiria Dar es Salaam (UWADAR) mhe. Mhagama alisisitiza kuwa Serikali haitawafumbia macho wamiliki wa vyombo vya usafiri ambao hawazingatii mikataba ya kazi kwa madereva.


“Ninaagiza mikataba ya maderva iangaliwe upya na ikiwezekana yaainishwe majina ya wamiliki wa magari wanaokiuka haki na sheria zilizopo za kuwapa madereva mikataba na stahiki zao ili sheria iweze kuchukua mkondo wake,”alisema Mhagama


Kutokana na changamoto mbalimbali za madereva zilizobainishwa wakati wa mkutano huo Mhe.Waziri aliwataka wajumbe wote kuangalia namna nzuri ya kukabili changamoto hizo ili kuhakikisha malalamiko ya madeva yanaisha na kufanya sekta hiyo kuwa na amani na utulivu.

“Lengo kuu ni kuona sekta ya usafirishaji inakuwa salama na yenye amani kwani ikumbukwe sekta hii ni nyeti, inabeba roho za watu wengi kila iitwapo leo kwa kuwasafirisha mikoani na nje ya mikoa.” Alisisitiza Mhagama.

Nae mwenyekiti wa Kamati hiyo Dkt. Leonard Chamuliho aliomba kamati kuyafikia maazimio ya muhimu yaliyojadiliwa na huku akisisitiza agizo la mhe. Mhagama la kuwataka wamiliki na waajiri wote kuzifuata na kuzitekeleza sheria za mikataba kwa waajiriwa wote.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post