Mbunge Asisitiza Mafisadi Wanyongwe Hadi Kufa

MBUNGE wa Nkasi Kaskazini, Ally Kessy (CCM) ambaye haishi vituko bungeni, amerudia kauli yake kwamba watu wanaothibitika kufanya ufisadi wa rasilimali za umma wanyongwe hadi kufa.





Akichangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, kwa mwaka wa fedha 2016/17, Kessy ambaye aliwahi kupendekeza mafisadi wauawe na makaburi yao yawekwe minyororo katika Bunge lililopita, alisema:

"Hakuna haja ya kuwapelekwa (mafisadi) mahakamani maana haiwezekani mtu ana nyumba 70 halafu unampeleka mahakamani.

"Hizo nyumba alipata wapi?”

Alisema kuwapeleka mahakamani mafisadi hakusaidii na alipendekeza wanyang’anywe nyumba na mali zote walizopata kwa njia za wizi na ukwepaji wa kodi.


Kuhusu mapato na matumizi ya Bunge, Kessy alisema wabunge wengi wanasafiri kama wakimbizi na alimsifu Rais Magufuli kwa kudhibiti safari za nje.

Alisema Rais ameanza kupigwa vita baada ya kuzuia ulaji wa watu na alisisitiza kuwa safari zisizokuwa na tija zipigwe marufuku, ili wabunge waishi kwa kufanya kazi majimboni kwao walikochaguliwa.

SUKARI

Akizungumzia hatua ya serikali kupiga marufuku uingizaji holela wa sukari kutoka nje, Kessy alisema ikataze pia uingizaji wa mchele unaotoka ng’ambo.

Kessy alishangaa kuwapo kwa mchele kutoka India na Thailand nchini, na kutaka fedha zinazoagiza nafaka hiyo ziokolewe kama ilivyofanyika kwenye sukari.

“Haiwezekani kuagiza mchele kutoka nje wakati mchele umerundikana Kyela, Tunduma, Sumbawanga... upigwe marufuku kama ilivyofanyika kwenye sukari,”alisema.

AKOSOA SERIKALI

Akichangia mada kwenye usafiri wa mwambao mwa Ziwa Tanganyika, Kessy alisema serikali ya awamu ya nne iliahidi meli mbili zingenunuliwa ziwani humo lakini anashangaa awamu ya tano inatangaza kukarabati meli ya Mv Liemba pekee.

Alisema Mv Liemba ina miaka 112 hivyo imechoka na kwamba inahitajika meli mpya ya kufanya kazi ziwani humo na siyo ukarabati.

Kwa upande wa uvuvi, aliomba wavuvi wafikiriwe na wawezeshwe kwani nchi jirani ya Zambia ina asilimia sita ya maji ya Tanganyika lakini ndiyo muuzaji mkubwa wa samaki na dagaa duniani.

Alisema Tanzania ina asilimia 38 ya Ziwa Tanganyika, lakini haijafanikiwa kwenye biashara hiyo.


Aidha, Mbunge wa Nkasi huyo alitaka utumbuaji majipu uwe kazi ya mara kwa mara na usisubiri Waziri Mkuu wala Rais pekee kufanya kazi hiyo.

UTUMBUAJI MAJIPU

Wakati Kambi ya Upinzani Bungeni ikisusia kuchangia hoja katika hotuba ya Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu, wabunge wa CCM wameendelea kuunga mkono utumbuaji majipu na kujinasibu kuwa kitendo hicho kinawapa hofu wapinzani.

Wabunge wa CCM hao wamemtaka Rais John Magufuli kutumbua majipu hadi ya wapinzani ili kuondoa matatizo kama hayo.

Wakichangia hotuba ya Waziri Mkuu, wabunge hao walisema utendaji wa Rais Magufuli haukutarajiwa na wapinzani hali inayowafanya kukosa hoja, na ndiyo maana wanasusa.

Mbunge Geita Vijijini Joseph Musukuma, alimuomba Rais atumbue majipu hadi upinzani kutokana na wenyewe kuwa ni majipu pia.

Alisema ni vyema wapinzani wakatumia akili kwa ajili ya kuwaletea maendeleo Watanzania badala ya kushauriana wasichangie bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu.

Aidha, Mbunge wa Mbinga Mjini, Sixtus Mapunda alisema kama serikali itawekeza katika viwanda hususan vile ambavyo uendeshaji wake umesuasua na vingine kufa, ajira kwa vijana na maendeleo yatapatikana.

Hata hivyo, alisema hotuba ya kambi ya upinzani haiwezi kujibu hoja ya Waziri Mkuu na Kiongozi wa Upinzani Freemon Mbowe, amepotosha Bunge.

“Nimuombe Mbowe akasome katiba vizuri na sheria ya bajeti, unapoongelea kutenga bajeti lazima uweke sheria ya kuisimamia," alisema Mapunda.

"Kuna kifungu cha sita cha sheria hii kinasema mamlaka ya serikali kubadilisha matumizi kwa kadiri atakavyoona inafaa kwa manufaa ya taifa.

“Kuchukua fedha zilizobaki kwenye mwezi Julai hadi Novemba, ambapo Bunge halikuwepo na fedha zikaenda kununua madawati hakuna kosa.”

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post