Angalia Picha!! Polisi Shinyanga Watangaza Vita na Waendesha Bodaboda,Masharti Kibao,Marufuku Kubeba Watoto



Kamanda wa Kikosi cha usalama barabarani Wilaya ya Shinyanga Vincent Msami akizungumza katika mkutano wa kikosi hicho na waendesha bodaboda mjini Shinyanga uliofanyika katika kituo cha mabasi yaendayo wilayani
 
Jeshi la Polisi wilaya ya Shinyanga limetangaza vita na waendesha bodaboda ambao wamekuwa sugu kwa kukiuka sheria za usalama barabarani huku wengi wao wakiendesha pikipiki hizo wakiwa wameshatumia vilevi hali ambayo imekuwa ikichangia kuongezeka kwa ajali nyingi.


Jeshi limetangaza vita hiyo kufuatia dalili za kuongezeka kwa ajali mwaka huu ambapo Tangu Januari hadi Machi mwaka huu tayari ajali za bodaboda zimeshatokea 21, vifo 15 na majeruhi sita ambao wamevunjika viungo mbalimbali vya miili yao, jambo ambalo ni hatari kupoteza nguvu kazi ya taifa.



Akizungumza juzi na waendesha bodaboda hao Kamanda wa Kikosi cha usalama barabarani Wilaya ya Shinyanga Vincent Msami alisema hawatavumilia kuona jeshi hilo linatumbuliwa majipu na rais kwa kushindwa kusimamia kikamilifu sheria za usalama barabarani na kukomesha ajali za bodaboda.


Msami alisema Jeshi hilo litaanza kuwakamata bodaboda ambao hawavai kofia ngumu,viatu, pikipiki kutokuwa na kadi, bima, leseni za uendeshaji, wanaotumia Vilevi ikiwamo na ubebaji wa mishikaki na kupakia watoto wadogo wenye umri chini ya miaka 10 kama abiria, na kubainisha watakao kamatwa na makosa hayo watafungwa jela.



Nao waendesha bodaboda hao walidai asilimia kubwa sheria hizo watazitekeleza isipokuwa la ubebaji wa watoto ambapo wengi wao wana tenda za kupeleka watoto shule na kuwarudisha Majumbani kwao, sehemu ambayo huwapatia pesa nyingi kuliko kukaa vijiweni ambapo hakuna abiria wa kutosha.



Walisema Jeshi la Polisi linapaswa kutowabana sana katika Sheria hizo likiwamo na Suala la Leseni ikiwa Vijana wengi wamejiajiri kupitia pikipiki hizo, bali waangalie utaratibu wa kuwapatia mafunzo ambayo yatawasaidia kupata Leseni kwa uharaka.




Walisema endapo jeshi hilo litawabana na kuanza kuwafunga, vijana wengi watarudi kwenye kazi zao za zamani na kuzalisha vibaka mitaani, wizi kuongezeka vitendo ambavyo kwa asilimia kubwa vilikuwa vimepungua, kwa sababu watakuwa hawana ajira huku wengine wakiwa tayari wameshaoa na wanafamilia. 
Stori na Marco Maduhu-Malunde1 blog

Bodaboda zikiwa katika eneo la kituo cha mabasi yaendayo wilayani mjini Shinyanga

Mkutano unaendelea

Afisa wa usalama barabarani akitoa elimu kwa waendesha bodaboda

Elimu inaendelea kutolewa












Picha zote na Emmanuel Mpanda

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527