UMOJA WA KLABU ZA WAANDISHI WA HABARI TANZANIA (UTPC) WATOA TAMKO KUHUSU MWANDISHI WA HABARI ALIYETEKWA HUKO ZANZIBAR KUELEKEA UCHAGUZI



Rais wa UTPC Deogratius Nsokolo

TAMKO LA UMOJA WA KLABU ZA WAANDISHI WA HABARI TANZANIA JUU YA KUTEKWA KWA MWANDISHI WA HABARI WA SAUTI YA UJERUMANI ( DW ) SALMA SAID.
 Salma Said mwandishi wa DW Zanzibar ametoweka baada ya kutekwa na watu ambao hawajafahamika jijini Dar es salaam, hali ambayo imeleta fadhaa na mshtuko kwa waandishi, jamii na familia yake hasa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi wa marejeo Zanzibar.
 Ifahamike kuwa Kazi ya mwandishi wa habari ni kutoa habari juu ya kila kinachoendelea katika jamii , hivyo kama kuna dosari , dosari hiyo ni ya jamii na sio ya anayeieleza dosari .
 UTPC inalaani na kupinga utekaji uliofanywa ambao sababu zake bado hazijulikani, hivyo tunaitaka serikali kuhakikisha Salma Said anatafutwa, kupatikana na anaachiwa huru mara moja kwa kuwa Serikali ndio yenye jukumu la kulinda raia wake.
 Kama utekwaji wa Salma umefanywa kutokana na kazi yake ya uandishi habari tunalaani vikali hatua hiyo, vitendo hivi havipaswi kuendelea katika nchi inayoheshimu misingi haki na Demokrasia, Vitendo vya namna hii vinadumaza na kufifisha uhuru wa habari . 
 Tunapinga kwa nguvu zetu zote waandishi wa habari kukamatwa na vyombo vya dola au makundi ya kihalifu kwa visingizio ama vya uchochezi au maslahi ya taifa.
 Waandishi tutaendelea kufanya kazi zetu bila kujali vitisho vya aina yoyote ile kutoka kwa mtu yoyote au Serikali. 

 Imetolewa na DEOGRATIUS NSOKOLO RAIS WA KLABU ZA WAANDISHI WA HABARI TANZANIA -UTPC. March 19, 2016.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527