JINSI WENJE ALIVYOVUKA KIKWAZO CHA MABULA KESI YA KUPINGA MATOKEO YA UBUNGE NYAMAGANA

Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza, jana ilitupilia mbali kwa gharama pingamizi lililowekwa na upande wa wakili wa mjibu maombi wa kwanza, Stanslaus Mabula, katika kesi ya kupinga matokeo ya ubunge wa jimbo la Nyamagana.

Kwa kutupwa pingamizi hilo lililowekwa na Mabula, mbunge wa sasa wa wa jimbo hilo, kesi hiyo itaanza kusikilizwa Jumatatu ijayo.

Jaji Kakusulo Sambo wa Mahakama Kuu Kanda Mwanza, alikubali kuahirisha shauri hilo baada ya kuridhika na sababu zilizotolewa na pande zote mbili, zikiomba kesi hiyo isikilizwe Machi 7, mwaka huu.

Upande wa mleta maombi ukiongozwa na wakili Elias Hezron, akisaidiana na Geofrey Kalaka, uliomba kuahirishwa kwa kesi hiyo baada ya wakili mwenzao mwandamizi, Deya Outa, kuugua. Waliomba muda wa kuandaa maombi mengine baada ya yale ya awali kutupiliwa mbali kwa gharama kutokana na kunukuliwa vibaya kwa vifungu vya sheria na kuiongoza vibaya mahakama.

Upande wa mjibu maombi namba moja (Mabula) aliyewakilishwa na wakili Constantine Mutalemwa akisaidiana na Faustine Malongo, waliiomba mahakama kuahirishwa kesi hiyo kutokana na kukubali sababu zilizotolewa na upande wa waleta maombi pamoja na wakili huyo (Mutalemwa) kusafiri kwenda jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kesi iliyoko katika Mahakama ya Rufani, hivyo kusababisha kutokuwapo jijini Mwanza.

Awali, Jaji Sambo alikubaliana na pingamizi lililowasilishwa mahakamani hapo na Wakili Mwandamizi wa Serikali Ajuaye Bilishanga, kuiomba mahakama kutupilia mbali maombi namba 8 ya mwaka 2016 kwa kuwa yalifunguliwa chini ya kifungu ambacho hakipo (kifungu cha 14 (1) sura ya 189 ambacho kilitakiwa kinukuliwe kifungu cha 89) hivyo kuiongoza vibaya mahakama, hivyo pingamizi la upande wa jamhuri lina mashiko na mahakama kukubaliana nalo na kulitupilia mbali kwa gharama.

Vilevile, ombi la upande wa mleta maombi la kutaka mahakama hiyo itoe ruhusa ya kupeleka maswali mawili kwa wajibu maombi wa kwanza na wa pili ambao wana nyaraka za fomu namba 21 (B) zilizotumika kwenye uchaguzi wa Oktoba 25, mwaka jana, yamekataliwa na mahakama haitotoa kibali cha maombi hayo. badala yake hatua ya utoaji kibali Itafanyika wakati kesi ya msingi imeshaanza kusikilizwa.

Shauri hilo lilikuwa likiendelea huku umati mkubwa wa wafuasi wa Wenje wakiwa wanasubiri nje ya mahakama. Baada ya uamuzi ya Jaji, umati huo ulilipuka kwa nderemo na vifijo na kushangilia huku wakiimba Wenje, Wenje na kulisukuma gari lake.

Jaji Sambo amezitahadharisha pande zote katika kesi hiyo kujiandaa na uhakika uwapo mahakamani hapo kwa ajili ya usikilizwaji wa awali wa shauri hilo ambalo amekusudia kulipeleka haraka ili kufikia uamuzi mapema, kabla ya kuanza vikao vya Bunge Juni, mwaka huu.

Wenje alifungua kesi hiyo dhidi ya Mabula, Msimamizi wa Uchaguzi Jimbo la Nyamagana, Kitia Sylvester na Mwanansheria Mkuu wa Serikali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post