MWANASHERIA MKUU WA SERIKALI NA ASKARI MAGEREZA WAWILI WAFIKISHWA MAHAMAKANI KWA KUMTOROSHA MTUHUMIWA WA MAUAJI YA ALBINO GEREZANI HUKO KATAVI



Jeshi la Polisi Mkoa wa Katavi limemfikisha mahakamani mwanasheria mkuu wa Serikali wa Mkoa wa Katavi na askari wa jeshi la magereza wawili wa gereza la mahabusu la Mpanda kwa tuhuma za kusaidia kumtorosha mtuhumiwa Alex Mayanza aliyekuwa akikabiliwa na kesi ya kujaribu kumuua Albino kwa kumkata kiganja cha mkono.


Kaimu kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Katavi Mohamed Rashidi aliwataja mbele ya waandishi wa Habari watuhumiwa hao kuwa ni mwanasheria Mkuu wa Serikali wa Mkoa wa Katavi Falhati Seif Khatibu na askari magereza wawili ambao ni A.5385 STG Deogratias Katani na A.287 S SGT John Masangula wa magereza la mahabusu la Mpanda Mjini .

Alisema jeshi la polisi lilipokea taarifa kutoka kwa raia wema hapo January 19 mwaka huukwamba mtuhumiwa Alex Manyanza aliyekuwa anakabiliwa na kesi Na Mto ,IR ,76,2015 ya kujaribu kuua mlemavu wa ngozi kwa kumkata kiganja cha mkono anayefahamika kwa jina la Limi Luchoma mkazi wa kata ya Maji Moto Wilaya ya Mlele kuwa hayupo kwenye gereza la mahabusu Mpanda.

Baada ya taarifa hizo jeshi la polisi lilianza upelelezi na kubaini mtuhumiwa huyo alitoroka tangu Januari 12 katika gereza la mahabusu la Mpanda ambapo hapo awali mtuhumiwa huyo aliwahi kutoroka wakati akiwa anatumikia kifungo katika gereza la kilimo la Kalilankulu kabla ya kukamatwa katika kesi hii ya kujaribu kuua Albino.

Jeshi la Polisi liliendelea na upelelezi wa kesi hiyo na ndipo ilipofika January 21 walipata taarifa kuwa mtuhumiwa Alex Mayanza anapatikana Mkoani Rukwa na baada ya taarifa hizo ufuatiliaji ulifanyika na kufanikiwa kumkamata mtuhumiwa Alex Manyanza akiwa amejificha katika kijiji cha Kipande Wilaya ya Nkasi Mkoa wa Rukwa.

Kaimu Kamanda Rashid alisema baada ya mahojiano ya kina mtuhumiwa alieleza jinsi alivyofanikisha mipango ya kutoroka gerezani akimtaja mjomba wake aitwaye Masanja Kashinje pamoja na rafiki yake Ngassa Mashindike ambao nao baada ya kukamatwa walikiri kufanya mipango ya kumtorosha kwa lengo la kuwafanya watuhumiwa wengine katika kesi kutotiwa hatiani akiwemo mjomba wake Masunga Kashinje.

Alisema walieleza waliwashirikisha askari magereza hao wawili na walikubaliana na kuwapatia kiasi cha shilingi milioni moja moja kwa kila askari hao ili kumwezesha mtuhumiwa Alex Manyanza kutoroka na pia walimtaja mwanasheria Mkuu wa Serikali wa Mkoa wa Katavi ambaye walidai walimpatia kiasi cha shilingi milioni mbili ili kumwondolea shitaka mtuhumiwa Masunga Kashinje baada ya kuwa mtuhumiwa Alex Manyanza kufanikiwa kutoroka gerezani .

Kaimu Kamanda wa polisi Rashid Mohamed alisema watuhumiwa hao wote watatu wamekishwa juzi katika mahakama ya Wilaya ya Mpanda kwa hatua zaidi za kisheria.


Na Walter Mguluchuma-Malunde1 blog Katavi

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527