WAFANYAKAZI ZAIDI YA 50 WA TANESCO WANUSURIKA KUFA BAADA YA GHOROFA KUPOROMOKA NA KUFUNIKA OFISI...




Zaidi ya wafanyakazi 50 wa shirika la umeme nchini, Tanesco mkoani Mbeya wamenusurika kifo baada ya vyuma vizito ambavyo vimetumika kutengenezea jukwaa la ujenzi wa jengo lenye urefu wa ghorofa 11 mali ya mfuko wa taifa ya bima ya afya kuporomoka na kufunika ofisi za Tanesco makao makuu ya mkoa wa Mbeya. 



Tukio hilo limetokea majira ya saa saba mchana baada ya mvua kubwa ya mawe ambayo imeambatana na upepo mkali kunyensha na kusababisha vyuma hivyo kuporomoka na kuangukia jengo la Tanesco hali ambayo imesababisha wafanyakazi wa shirika hilo kupatwa na hofu kiasi cha kuondolewa haraka ndani ya jengo hilo kama ambavyo meneja wa Tanesco mkoa wa Mbeya anavyoelezea.

Meneja huyo wa Tanesco mkoa wa Mbeya amesema tukio hilo limesababisha hasara kubwa kwa kampuni, ikiwa ni pamoja na uharibufu wa jengo na watumishi kushindwa kufanya kazi.

Baadhi ya wafanyakazi wa Tanesco wamesema kuwa tukio hilo ambalo limetokea wakiwa kazini ndani ya jengo hilo limewasababishia mshtuko mkubwa huku wakidai kuwa tangu kuanza kwa ujenzi huo kumekuwepo na matukio yanayo hatarisha maisha yao kutokana na wakandarasi wanaojenga jengo hilo kutokuwa makini.

Mkandarasi wa kampuni ya Y&P Architect (T) LTD inayojenga jengo hilo alipoona camera ya ITV aliamua kutimua mbio, huku meneja wa wakala wa usalama mahali pa kazi kanda ya nyanda za juu kusini, George Chali akikataa kuzungumzia suala hilo kwa madai kuwa amekatazwa kusema lolote na mabosi wake.

 Via>>>ITV

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post