Hatari!! NDEGE YAANGUKA NA KUUA ABIRIA WOTE ZAIDI YA 200 WALIOKUWA KWENYE NDEGE HIYO



Watu 224 wamefariki baada ya ndege ya shirika moja la Urusi kuanguka katika eneo la Sinai nchini Misri.

Ndege hiyo aina ya Airbus A-321 ilikuwa imetoka mji wa Sharm el-Sheikh ikielekea mji wa St Petersburg nchini Urusi ilipoanguka.

Maafisa wa serikali wa Misri wamenukuliwa na shirika la habari la AP wakisema hakuna manusura wowote waliopatikana.

Maafisa wa usalama eneo hilo wameambia shirika la habari la Reuters kwamba kufikia sasa miili 150 imepatikana.

Rais wa Urusi Vladimir Putin ametuma risala za rambirambi kwa jamaa za waathiriwa na kuagiza uchunguzi ufanywe.

Ujumbe kutoka Urusi ukiongozwa na Waziri wa Uchukuzi Maksim Sokolov umeelekea eneo la mkasa huku Rais wa Misri Abdel Fattah el-Sisi naye akirejea nyumbani kutoka Bahrain.

Awali, kulikuwepo na utata kuhusu hatima ya ndege hiyo, baadhi ya ripoti zikisema ilitoweka karibu na visiwa vya Cyprus. Lakini Ofisi ya Waziri Mkuu wa Misri Sharif Ismail imethibitisha kwamba ndege hiyo ilianguka katikati mwa eneo la Sinai.

Afisi hiyo imeongeza kuwa Bw Ismail ameunda kamati ya dharura ya kushughulikia ajali hiyo.

Wengi wa abiria walio kwenye ndege hiyo ni watalii kutoka Urusi.

Ndege hiyo ni ya shirika la ndege la Kogalymavia. Ripoti za karibuni zinasema ilikuwa imewabeba abiria 217 na wahudumu saba.



Shirika la Urusi linalosimamia safari za ndege Rosaviatsiya limesema ndege hiyo safari nambari 7K 9268 iliondoka Sharm el-Sheikh saa 06:51 saa za Moscow (0:351 GMT) na ilitarajiwa kuwasili uwanja wa ndege wa Pulkovo mjini St Petersburg saa 12:10.

Waliongeza kuwa ndege hiyo ilikosa kuwasiliana na wasimamizi wa safari za ndege Cyprus dakika 23 baada ya kupaa kama ilivyoratibiwa na ikatoweka kutoka kwenye mitambo ya rada.

Ubalozi wa Urusi nchini Misri umesema ndege hiyo ilijaribu kutua katika uwanja wa ndege wa El Arish.

Kituo maalum kmefunguliwa uwanja wa ndege wa Pulkovo kusaidia jamaa za abiria waliokuwa kwnnye ndege hiyo, shirika la habari la Tass limesema likinukuu maafisa wa jiji la St Petersburg.

Kundi la Kiislamu la Islamic State (IS) limedai kuhusika kuangusha ndege hiyo. Eneo ambalo ndege hiyo ilianguka limekumbwa na maasi ya kundi la Sinai Province ambalo lina ushirika na kundi la IS.

Maafisa wa usalama Misri hata hivyo walikuwa awali wamesema ajali hiyo ilisababishwa na hitilafu za kiufundi na kwamba ni vigumu kwa waasi hao kwa kutumia makombora.
Via>>>BBC

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527