Jeshi
la Polisi mkoani Tabora limefanikiwa kumtia mbaloni mtu mmoja
aliyejulikana kwa jina la Masanja Mwinamila, mkazi wa kijiji cha Konanne
kata ya Ugembe wilayani Nzega mkoani Tabora, akiwa katika harakati za
kutafuta soko la kumuuza mlemavu wa ngozi (Albino) mtoto wa dada yake
kwa fedha nyingi.
Akitoa taarifa kwa vyombo vya habari mkoani Tabora kaimu kamanda wa
polisi mkoani Tabora kamishina msaidizi Juma Bwire amemtaja mtuhumiwa wa
tukio hilo kwa jina la Masanja Mwinamila, ambaye aliangukia katika
mikono ya polisi kutokana na taarifa za wasamaria wema, na polisi kuweka
mtego.
Aidha kaimu kamanda wa polisi Juma Bwire amesema fedha alizo
taja kumuuza binti huyo, idadi imehifadhiwa isiwe kichocheo, huku akidai
kuwa, wanaendelea kumuhoji kama kuna watu anaoshirikiana nao.
Mama mzazi wa mtoto huyo aliyenusurika Magreth Hamis (miaka sita)
ambaye pia ni mlemavu wa ngozi, amesema kuwa, katika nyumba yao anaishi
na watoto wake kutokana na kufiwa na mmewe walivamiwa na watu waliokuwa
wameficha nyuso zao na kuanza kuwafukuza na kisha kumkamata mtoto huyo
na kutokomea naye.
Aidha kaimu kamanda Juma Bwire ameitaka jamii kutoa ushirikiano
pale wanapobaini watu wanaosababisha walemavu wa ngozi kuishi kwa
wasiwasi ili kukomesha vitendo vya ukatili.
Via>>ITV