Hatari!! MTOTO AFARIKI BAADA YA KUTUMBUKIA KWENYE KARO LA CHOO HUKO KAHAMA!!


Mtoto mmoja Reuben Daud(3) mkazi wa Nyihogo wilayani Kahama mkoani Shinyanga amefariki dunia leo baada ya kutumbukia kwenye karo la choo ambapo mazingira ya tukio hilo hayakufahamika.

Kwa mujibu wa mashuhuda wa tukio hilo wamesema mnamo saa 3 ya asubuhi kulizagaa taarifa ya kupotea kwa mtoto katika eneo hilo na ndipo jitihada za kumtafuta zikafanyika na kumkuta akielea kwenye karo la choo nyumba ya jirani amefariki.

Mmoja wa mashuhuda hao Khalfan Mohamed ameelezea tukio hilo kuwa alisikia taarifa za kupotea kwa mtoto ambapo baadae taarifa za kupatikana kwa mtoto huyo akiwa ameelea kwenye karo, hivyo taratibu za kuuopoa mwili zikafanyika. 

Kwa upande wa baba mzazi wa mtoto huyo Daud Reuben ameelezea tukio hilo kuwa mtoto aliondoka kwenda kununua kitafunwa kwa ajili ya chai lakini hakurudi ndipo walipowashirikisha majirani kumtafuta ambapo walimuona kwenye karo hilo akiwa amefariki.

Naye mtendaji wa mtaa huo Simon Mabumba amesema uzembe wa kuacha makaro wazi ndiyo chanzo cha matukio kama hayo kuendelea kujitokeza hivyo wananchi wanapotaka kujenga wanapaswa kuzingatia usalama wa jamii na si kuangalia shughuli zao tu. 

Jeshi la Polisi wilayani Kahama lilifika katika eneo la tukio na kuuchukua mwili wa marehemu na kisha kuupeleka chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali ya wilaya ya Kahama kwa ajili ya uchunguzi zaidi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527