ASILIMIA 50 YA WATOTO YATIMA WANALELEWA NA WAZEE WA MIAKA ZAIDI YA 60 NCHINI TANZANIA



Imebainishwa kuwa asilimia 50 ya watoto yatima katika jamii wanalelewa na wazee wenye umri wa zaidi ya miaka 60 hali ambayo inasababisha wazee kuendelea kuishi maisha magumu na kunyanyasika na kupoteza haki zao za msingi.

Hayo yamebainishwa juzi na mratibu wa Chama Cha Wataalam Viongozi Wanawake wa Kilimo na Mazingira (TAWLAE) Eliasenya Nnko(PICHANI) wakati wa kikao cha Waandishi wa Habari klichofanyika mjini Shinyanga kuhusu kuongeza na uhamasishaji juu ya sera ya mikakati ya kuboresha maisha ya wazee nchini.

Nnko alisema takwimu zinaonesha kuwa asilimia 80 ya wazee wanaishi vijijini huku 50% ya watoto yatima wanatunzwa na wazee hususani wazee wanawake kutokana na vijana kutekeleza watoto wazo na kukimbilia mjini kwa sababu mbalimbali ikiwemo kisingizo cha kutafuta maisha.

Alisema sababu nyingine ya watoto yatima kulelewa na wazee ni kutokana na vifo vya wazazi vinavyotokana na magonjwa ya kuambukiza ikiwemo UKIMWI.

Katika hatua nyingine alisema wazee nchini wanakabiliwa na changamoto ya ukiukwaji wa haki za wazee kama vile mauaji na unyanyasaji wa wazee ikiwemo kupoteza mali zao,kupigwa,kupuuzwa na kutolewa maneno ya kashfa sambamba na kufukuzwa kwenye maeneo yao.

Nnko aliongeza kuwa bado wazee wanabaguliwa katika taasisi za fedha kwa kunyimwa mikopo ama mitaji ingawa asilimia 63 ya ardhi yote nchini inamilikiwa na wazee kitendo ambacho kinasababisha waendelee kuishi maisha duni.

Alisema kikwazo kikubwa kinatokana na mtizamo hasi wa jamii kwa wazee,sera ya matamko kuhusu wazee kutotungiwa sheria,kukosa uwakilishi katika vyombo vya maamuzi na baadhi ya wenye mamlaka kutopenda kuwapatia wazee hata yale yaliyo kwenye sera na miongozo ya taifa.

Kwa upande wake afisa Maendeleo ya Jamii na Vijana katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Daudi Kisangure alisema katika kukabiliana na suala la wazee kulea watoto yatima serikali inaendelea kutoa elimu kwa jamii kuhusu kujiunga na vikundi vya uzalishaji mali ili kuwafanya vijana wasikimbilie mjini bali wabaki vijijini kwani watakuwa na kipato.

Kisangure alisema changamoto kubwa katika kukabiliana na masuala ya wazee katika wilaya ya Shinyanga ni ufinyu wa bajeti ukilinganisha na makundi mengine kama vile vijana na wanawake ambao hutengewa asilimia 5 kupitia mapato ya ndani ya halmashauri husika.

Naye mganga mkuu wa wilaya ya Shinyanga Dkt Emmanuel Kadelya Joha alisema ili kumaliza tatizo la changamoto ya huduma za afya kwa wazee tayari jumla ya wazee 3000 kati ya 11,000 wamepigwa picha na watapatiwa vitambulisho katika awamu ya kwanza.

Alisema zoezi la kuwapatia wazee vitambulisho kwa ajili ya matibabu ni endelevu na wazee wanaendelea kujaza fomu katika ofisi za vijiji na kata ili kuhakikisha kuwa hawapati usumbufu wanapofika katika vituo vya afya na hospitali.
 
Na Kadama Malunde-Shinyanga

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527