Wananchi watatu
kati ya kumi (30%) wamesha kukumbana na wizi ndani ya kipindi cha mwaka jana.
Kwa ujumla, nusu ya Watanzania wote wamewahi kuibiwa.
Asilimia 84 ya wananchi wanaamini kuwa kuna
uwezekano wa wao kuathiriwa na makundi ya vijana wahalifu kama Panya Road.
Mwezi Januari 2015, Panya Road ilileta wasiwasi mkubwa jijini
Dar es Salaam kwa kufanya vitendo vya uhalifu na vurugu, tukio hili lilitawala
mijadala kwenye mitandao ya kijamii na kupelekea mamia ya vijana hao kukamatwa.
Wananchi sita kati ya kumi (60%) kitaifa wamewahi kusikia kuhusu Panya Road lakini karibu wananchi tisa
kati ya kumi (87%) walisema hakuna kikundi kama hicho katika maeneo yao.
Wananchi wawili kati ya kumi (18%) wameripoti
kuwa walishuhudia ghasia wakati wa uchaguzi wa serikali za mitaa mwezi Desemba
2014.
Matokeo haya yametolewa
na Twaweza kwenye muhtasari wake wa utafiti wenye jina la Je, tuko Salama?
Maoni ya wananchi juu ya usalama na haki.
Muhtasari huu umetokana na
takwimu za Sauti za Wananchi, utafiti wa kwanza Afrika wenye uwakilishi
wa kitaifa unaofanyika mara kwa mara kwa njia ya simu ya mkononi.
Takwimu hizi zilikusanywa
kwa wahojiwa 1,401 kutoka Tanzania Bara (Zanzibar haimo katika matokeo haya) mwezi
Februari na Machi 2015.
Licha ya kuongezeka kwa matukio ya vurugu
za kisiasa pamoja na wizi na hofu juu ya makundi ya vijana wahalifu, wananchi nane
kati ya kumi (79%) walisema hawajawahi kabisa, au wamewahi mara chache kujihisi
kutokuwa salama katika jamii zao na maeneo wanayoishi.
Hata hivyo, wananchi wanaamini kuwa mfumo
wa sheria haufanyi kazi ipasavyo.
Zaidi ya nusu ya wananchi (53%) wanaamini kuwa
mwananchi wa kawaida ataadhibiwa kwa mujibu wa sheria akitenda kosa.
Lakini kuadhibiwa
kwa watu wenye kipato cha chini ni vigumu sana.
Wananchi wachache (14%) wanaamini
kuwa watu wenye kipato cha juu wanaweza kuadhibiwa iwapo wanavunja sheria, na wengine
(21%) wanaona hili pia linawezekana kwa watumishi wa umma.
Idadi hii imeshuka ukilinganisha
na takwimu za mwaka 2013 ambapo asilimia 39 ya wananchi walidhani kuwa watumishi wa umma watakumbana
na mkono wa sheria wanapotenda makosa.
Pamoja na haya yote, wananchi sita kati
ya kumi (60%) wanaamini jeshi la polisi linawahudumia zaidi watu wenye pesa
kuliko watanzania wa kipato cha chini.
Licha ya kuwa na imani kwamba polisi
wanapendelea matajiri, wananchi wanne kati ya kumi (37%) waliripoti kwenda polisi
wanapokumbana na uhalifu.
Idadi hiyo hiyo (32%), wanategemea vikundi vya ulinzi
vya kijamii au kamati zao za kijiji/mtaa.
Baadhi hawaendi kutoa taarifa polisi
kwa sababu ya rushwa (29%), na wengine kwasababu polisi hawatawajali (14%).
Inaonekana
kwamba matukio ya ukatili dhidi ya polisi yameongezeka.
Wananchi wawili kati ya
kumi (21%) wameyasikia matukio ya aina hii. Mwaka jana (2013) ni mwananchi
mmoja tu kati ya kumi aliyeyasikia matukio kama haya.
Kutokana na imani ndogo na jeshi la polisi
kama wanavyoripoti wananchi, watu wengi wameanzisha vikundi vya usalama vya kijamii
ambavyo husimamia utekelezaji wa sheria za kawaida.
Taarifa nyingi za uhalifu
na vurugu zinapelekwa huko, huku wananchi watatu kati ya kumi (29%) wakiripoti
kuwahi kusikia matukio ya vitisho, watu kupigwa na vikundi hivi vya usalama.
Elvis Mushi,
Meneja
wa Sauti za Wananchi alisema "Wananchi wanakabiliwa na wizi, hofu
ya magenge na kukosekana kwa usalama ifikapo kipindi cha uchaguzi. Pia wanahisi
kwamba vyombo vya sheria vinaupendeleo. Hii ni changamoto kwa watunga serikali.
"
Aidan
Eyakuze, Mkurugenzi Mtendaji wa Twaweza, aliongeza kwa kusema " Kwanza,
wananchi wengi wanajihisi kuwa salama katika maeneo yao lakini bado wanakumbana
na vitendo vya wizi, wanaogopa kuvamiwa na vikundi kama Panya Road na baadhi
yao kushuhudia ghasia na vurugu za kisiasa.
Aidha, wananchi wameshuhudia ongezeko
la ukatili dhidi ya vituo vya polisi ndani ya miaka miwili iliyopita, jambo
hili linapunguza imani yao na vyombo vya usalama.
Usalama una umuhimu wa
kipekee katika masuala ya kijamii na kiuchumi. Rai yetu ni kwa serikali
kuyazingatia maoni haya ya wananchi katika utekelezaji wa jukumu lake la
kuwahakikishia wananchi usalama wa hali na mali."