WANAWAKE WA KIMASAI WAANGUA VILIO BAADA YA KUIBIWA NG'OMBE WAO

Wanawake wajane ambao ni Wafugaji jamii ya Kimasai, wamejikuta wakiangua kilio katika kituo cha Polisi Mvomero, mkoani Morogoro baada ya kukabidhiwa idadi pungufu ya ng'ombe zilizokamatwa baada ya kuporwa na kundi la ulinzi wa jadi la wakulima. 

Walinzi hao wa jadi kutoka katika kijiji cha Dihombo, lilivamia Kijiji cha Kambala ambacho wanaishi wafugaji hao na kupora ng'ombe 145 kwa madai kuwa wafugaji wa kijiji hicho kuwapora wakulima wenzao pikipiki tatu na kusababisha uhalibifu wa trekta wakati wakielekea shambani katika bonde la Mgongola na pikipiki hizo kutelekezwa porini. 
Mmoja wa wanawake hao, Belitha William, alisema akiwa kijijini  Kambala akiendelea na shughuli za kuchunga mifugo yake, ghafla alivamiwa na kundi la vijana wenye silaha za jadi maarufu kama muano na kupora ng'ombe wake wapatazo 145 pamoja na ndama na kuondoka nao. 
Alisema baada ya kuona kundi hilo la vijana yeye na familia yake na wafugaji wengine walikimbia katika eneo hilo kwa ajili ya kusalimisha maisha yao na ndipo kundi hilo likamua kuondoka na mifugo hiyo na kwenda nayo katika ofisi ya kijiji cha Dihombo.
Mfugaji huyo alisema alipoifuatilia mifugo hiyo alielezwa inalindwa na kundi la walinzi wa jadi mpaka pale wafugaji wa jamii hiyo ya kimasai watakaporudisha pikipiki walizopora wafugaji wenzao.  
Hata hivyo, alisema baadaye mifugo hiyo ilipelekwa ofisi ya Tarafa ya Mvomero kwa ajili ya kupigwa faini mifugo hiyo kuzurura katika mashamba huku mingine ikiwa haipo. 
Kwa upande wao, wakulima walioporwa pikipiki hizo, Fabian Clement pamoja na Francis Boniface, wakielezea tukio la kuporwa pikipiki hizo, walisema kwa nyakati tofauti kuwa wakati wakielekea katika mashamba ya bonde la Mgongola kwajili ya kuwapelekea chakula wenzao, waliona kundi kubwa la wafugaji jamii ya Wamasai wakiwa na silaha za jadi pamoja na bunduki  likiwafuata ndipo walipokimbilia porini.
Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Mussa Malambo, alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa baada ya polisi kupata taarifa hizo walifanikiwa kwenda katika eneo hilo na kuwataka wakulima hao kuzifikisha ng'ombe hizo katika ofisi ya Tarafa na tayari mwenye ng'ombe hao wamekabidhiwa baada kupigwa faini.

Na Ashton Balaigwa  -Nipashe

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post