WANANCHI WALALAMIKIA MGODI WA BULYANHULU KUTIRIRISHA MAJI YENYE SUMU


Taswira eneo la mgodi wa Bulyanhulu-Kahama

Wananchi wa kijiji cha Namba Tisa katika kata ya Bulyankulu wilayani Kahama Mkoa wa Shinyanga wameulalamikia mgodi wa Dhahabu wa Bulyanhulu kwa kutiririsha maji yenye sumu ya sayanaidi (CYANIDE) kwenye mashamba yao.
Hayo yamebainishwa jana na Wananchi wa kijiji hicho, kwenye mkutano wa hadhara mbele ya Mkuu wa wilaya hiyo Benson Mpesya ambapo mkutano huo ulikuwa na lengo la kujadili athari za sumu hiyo.


Wananchi hao walisema maji hayo ya sumu yameathiri mazao yao, waliyokuwa wamelima kwa ajili ya chakula na biashara, jambo ambalo walisema linawarudisha nyuma kimaendeleo.


“Ndugu Mkuu wa wilaya sisi kama wananchi wa kijiji hiki tulikuwa tumelima mpunga, nyanya, na tulikuwa tumepanda miti ya matunda lakini vyote vimekauka kutokana na sumu inayotoka mgodini ,tunaomba utusaidie kwa hilo,”walisema wananchi hao.

Walisema kutokana na sumu hiyo kuzagaa kila mahala ,wamekuwa wakipata shida kubwa sehemu ya kunyweshea  mifugo yao, hivyo wameiomba serikali iingilie kati suala hilo.


“Jambo hili limetuathiri sana wafugaji, kwani hatuna sehemu ya kunyweshea mifugo yetu, hali inayotulazimu tuuze mifugo yetu kwa hasara kwa wachinjaji wa nyama, ili mifugo hiyo isife kwa kukosa maji”,waliongeza wananchi hao.


Baada ya kupokea malalamiko hayo Mpesya, aliwaomba wananchi hao wawe watulivu wakati serikali inalishughulikia suala hilo kwa muda mfupi na kuwataka wananchi wasitumie maji hayo kwa shughuli yeyote.


“Kwanza nimejionea mwenyewe jinsi sumu ilivyozagaa na mazao yenu yalivyokauka na kuharibika poleni sana kwa hilo, lakini nalishughulikia ndani ya muda mfupi suala hili litaisha, na malalamiko yenu nimeyasikia na kuyapokea ila naombeni msitumie maji haya kwa shughuli yeyote iwe kunywa, kuoga wala kupikia ni hatari sana”,alisema Mpesya.


Kwa upande wake Msemaji wa Mgodi huo Abdallah Msika, alikiri kuwepo kwa sumu hiyo kuzagaa kwenye mashamba ya wananchi hao, ambapo alisema kuzagaa kwa sumu hiyo kulisababishwa na mvua kubwa kunyesha hali iliyopekea bwawa la mgodi huo kujaa maji na kutiririsha mpaka kwenye mashamba.


Hata hivyo Afya za wakazi wa kijiji hicho, ziko hatarini kutokana na maji hayo ya sumu ya Sayanaidi (CYANIDE), ambapo watu 15 wamebabuliwa ngozi zao na sumu hiyo hatali kabisa.

Na Valence Robert-Malunde1 blog Kahama

Bonyeza hapa Tukupe habari zote mara moja zikitoka "HABARI" VITUKO "MAPENZI"MAGAZETI,UDAKU>
Endapo una Habari,Picha,Video,Tangazo au Tatizo Lolote wasiliana nasi kwa namba  +255 688 405 951

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post