Wananchi wa kijiji cha Puma katika wilaya ya Ikungi mkoani Singida
wamemkataa mwenyekiti wa kijiji hicho katika mkutano wake wa kwanza na
kusababisha diwani wa kata hiyo kwa kushirikiana na jeshi la polisi
kuingilia kati na kufunga mkutano kabla ya wakati ili kumnusuru asipigwe
na wananchi.
Wananchi hao waliokuwa na hasira wamesema hakuna sababu ya
kuwa na mwenyekiti ambaye wananchi hawamkubali kwa sababu katika
uchaguzi uliopita kulikuwa na udanganyifu katika upigaji kura.
Kutokana
na hali hiyo wamesema ni bora kuachana na vyama vya siasa wachague
mwenye kiti wa kimila ili kukisaidia kijiji cha Puma kupata maendeleo.
Baada ya vurugu kuongezeka diwani wa kata hiyo kwa tiketi ya
CCM,Bwana Ramadhani Kulungu ilibidi kufunga kikao hicho ili kuweza
kumnusuru mwenyekiti wa kijiji cha Puma na kuwatuliza wananchi
ili kusitokee uvunjifu wa amani.
Mwenyekiti wa kijiji cha Puma kwa tiketi ya CCM ,Bwana Sifa Joramu
awali ambaye alishindwa kabisa kuendesha kikao chake ,baada ya jeshi la
polisi kuingilia kati na kuamua kumsindikiza kwa ulinzi mkali huku
wananchi wakimzomea na kusema hawamtaki,amesema hizo ni fujo za vyama
vya upinzani lakini yeye atahakikisha kazi anafanya kwa sababu yeye
ndiye aliyeshinda na kuapishwa kwa kazi ya uwenyekiti wa kijiji cha Puma.
Kundi la watu waliamua kumfuata na kumbeba juu kisha kumzungusha mitaani Bwana Hassan
Chaimbo aliyegombea kwa tiketi ya CHADEMA na kushindwa kwa kupata kura
mianne arobaini na nne dhidi ya Bwana Sifa Joramu alishinda
uenyekiti wa kijiji cha Puma kwa tiketi ya CCM katika uchaguzi
uliofanyika mwishoni mwaka jana na kupata kura mianne hamsini na saba.
via>>ITV