Mtoto
mchanga mwenye umri wa mwezi mmoja, Yadiko Chigoda amelazwa katika
Hospital ya Benjamini Mkapa Wilayani Mpwapwa Mkoani Dodoma baada ya
kupigwa na mchi kichwani na baba yake mzazi na kumsababishia maumivu
makali.
Akizungumza mama mzazi wa
mtoto huyo, Carolina Mnyawami ambaye ni mkazi wa kijiji cha Mingui kata
ya Lumuma Wilayani Mpwapwa amesema tukio hilo limetokea jana majira ya
saa 4 asubuhi ambapo mume wake aliyefahamika kwa jina la Fabian Chigoda
alikuwa anapigana na kaka yake hivyo aliamua kuwaamulia ugomvi wao.
Amesema katika ugomvi huo
walikuwa wanapigana na fimbo, hivyo alipowanyang’anya fimbo hiyo ili
wasiendelee kupigana ndipo (Chigoda) alipoamua kuchukua mchi ili ampige
nao mkewe kichwani lakini alikwepa na alipourusha ndipo ulipompata mtoto
huyo kichwani.
“Nilipowanyang’anya fimbo
ili wasiendelee kupigana, mume wangu aliokota mchi na kunirushia
kichwani.. kwa bahati nzuri niliuona mchi huo na kukwepa ili usinipige
ndipo ulipompiga kichwani mwanangu niliyekuwa nimembeba mgongoni,”
amesema Carolina.
Ameongeza kuwa, “Baada ya kuona kuwa amempiga mtoto alikimbia na hajulikani alipo mpaka sasa.”
Mganga Mkuu wa Wilaya ya
Mpwapwa, Said Mawji amethibitisha kumpokea mtoto huyo na kwamba hivi
sasa mtoto huyo anaendelea kupata tiba na uchunguzi zaidi wa afya yake.
“Ameumia sana kichwani
lakini bado tunampatia tiba na uchunguzi zaidi kwenye fuvu la kichwa,
kwani inaonekana kama vile limepasuka,” amesema Dk, Mawaji.
Hata hivyo amesema kuwa
wanafanya mpango wa kumpa rufaa mtoto huyo ili aweze kwenda kutibiwa
katika hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
Ofisa Mtendaji wa Kijiji
cha Mingui, Mwingwa Udoba amesema chanzo cha tukio hilo ni ugomvi wa
kifamilia na kwamba bado wanamtafuta baba mzazi wa mtoto huyo kwa kuwa
alikimbia baada ya tukio hilo.
Kamanda wa polisi Mkoa wa
Dodoma, David Misime alipotafutwa kuzungumzia tukio hilo simu yake
ilipokelewa na mtu aliyesema kuwa Kamanda alikuwa kwenye kikao cha kazi.