VIONGOZI WA SERIKALI ZA VIJIJI NA MAKAMANDA WA SUNGUSUNGU MNASIMAMIA MAUAJI YA RAIA



Jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga limesema matukio ya kujichukulia sheria mkononi katika maeneo mbalimbali mkoani hapa  yanasababishwa na baadhi ya viongozi wa serikali za vijiji na makamanda wa sungusungu kuhusika katika kusimamia mauaji hayo kwa matendo na kauli zao.

Hayo yamesemwa na kamanda wa polisi mkoani hapa ACP Evarist Mangala mwishoni mwa wiki hii katika kongamano  la vikundi vya ulinzi shirikishi sungusungu” mkoa wa shinyanga lililofanyika katika ukumbi wa VETA mjini hapa ambalo lilikutanisha wadau mbalimbali wa maendeleo wakiwemo viongozi wa dini.

“Viongozi hawa wamehusika kusimamia mauaji hayo kwa matendo na kauli zao badala ya kuwaelimisha wananchi kutojichukulia sheria mkononi,na pindi jeshi la polisi linapofika eneo la tukio hukuta mtuhumiwa kauawa na linapouliza nani kahusika katika mauaji huambiwa kauawa na yowe maarufu kama mwano, sasa unajiuliza yowe ni nani,lakini jibu ni binadamu hao hao”, Mangala alisema.

Akizungumzia kuhusu mauaji yanayotokana na imani za kishirikina,ingawa kwa miaka ya hivi karibuni yanaonekana kupungua,alisema uchunguzi unaonesha kuwa waganga wa jadi wanaojihusisha na upigaji wa ramli chonganishi wamehusika zaidi kuendeleza uwepo wa mauaji dhidi ya vikongwe na walemavu wa ngozi, Albino.

Hata hivyo alisema bado kuna changamoto katika mauaji hayo kutokana na sababu kuwa yapo ndani ya jamii au familia zaidi ,ambapo ndugu wa aliyeuawa wamekuwa wahusika au wanajua wauaji wa ndugu yao, lakini hawasemi na wanalifanya suala hili kuwa la siri.

“Wanajamii wa eneo husika mkiwemo makamanda wa sungusungu na wenyeviti wa serikali za vijiji nyie mmekuwa sehemu ya kuficha siri hizo, nawasisitiza kusema ukweli popote na kwa jambo  lolote la kisheria”,Kamanda Mangala alisisitiza.

Kwa upande wake mkuu wa upelelezi wa makosa ya jinai mkoa wa Shinyanga ACP Hussein Kashindye alivitaka vikundi vya ulinzi shirikishi yaani sungusungu vilivyoanzishwa na kufundishwa kutii sheria za nchi,kutambua wajibu na miiko ya kazi yao ili kupunguza au kuzuia matukio ya uhalifu katika jamii.

“Wajibu na miiko ya sungusungu na ile ya askari polisi haitofautiani ,kwani wote tunakatazwa kuulinda uhalifu na wahalifu waliopo katika maeneo yetu, na badala yake tunawajibika kuwataja hadharani ili sheria ichukue mkondo wake”,Kamanda Kashindye alisema.

Katika hatua nyingine aliwatahadharisha na kuwakumbusha kuwa mhalifu naye ana haki yake,na haki hiyo inapatikana mahakamani tu na si vinginevyo,hivyo mhalifu anapokamamtwa apelekwe polisi na polisi nao hawawezi kumhukumu bali watampeleka mahakamani.

Aidha aliwaagiza wakuu wa upelelezi wa wilaya zote mkoani hapa kufanya zoezi la kuwapiga picha makamanda wa sungusungu na viongozi wa  vijiji vyote ikiwa ni pamoja na kuchukua alama zao za vidole ili jeshi la polisi litambue viongozi wahalifu wanaojificha katika vikundi hivyo vya ulinzi shirikishi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments