
Wachimbaji wadogo wa madini katika mgodi wa Mwakitolyo, Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga wamesema kutozwa tozo mpya ya Sh200,000 kwa kila gari linalobeba mawe kutoka mgodini ni kuwaumiza kutokana na kulipa tozo zingine ambazo ziko kwa mujibu wa sheria.
Hatua hiyo imekuja kufuatia malalamiko kutoka kwa wachimbaji wadogo mgodi wa Mwakitolyo, waliodai kutozwa Sh 200,00 kwa kila gari linalotoka mgodini likiwa na mawe kwani hatua hiyo imekuwa mzigo mkubwa unaowaathiri kiuchumi na kudhoofisha shughuli zao za kila siku.
Wakitoa malalamiko yao kwenye kikao cha Mkuu wa Wilaya , wachimbaji wameeleza kuwa pamoja na tozo hiyo mpya, tayari wanakabiliwa na gharama nyingi za uendeshaji ikiwemo mrabaha, huduma mbalimbali, michango ya kijamii pamoja na ada za ukaguzi.
Mchimbaji mdogo Alphonce Magesa, amesema hali ya uzalishaji imekuwa ngumu zaidi kutokana na gharama hizo, akibainisha kuwa mazingira ya mgodi huo yanahitaji uwekezaji mkubwa wa uendeshaji kila siku.
Alieleza kuwa matumizi ya mashine kama greda pamoja na mafuta kwa kiwango kikubwa vinaongeza mzigo, hali inayowafanya wachimbaji kushindwa kupata faida inayotarajiwa .

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa wachimbaji wadogo wilayani humo, Elias Amos, amesema suala la tozo limekuwa likilalamikiwa kwa muda mrefu bila kupatiwa ufumbuzi wa kudumu, hivyo kuhitaji uamuzi wa haraka wa mamlaka husika.
Akifafanua zaidi, Mtatiro amesema tozo hiyo ilipitishwa na Kamati ya Fedha na Mipango mwaka 2022 na kuidhinishwa na Baraza la Madiwani kabla ya kuanza kutekelezwa mwaka huu,ambapo ametoa maagizo ipitiwe upya ili kuondoa malalamiko.
Amesema lengo la Serikali si kuwaumiza wananchi bali kuhakikisha kunakuwa na uwiano kati ya ukusanyaji wa mapato na ustawi wa wadau wa sekta ya madini.




Social Plugin