Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

VIONGOZI WA DINI SHINYANGA WATOA TAMKO KUELEKEA UCHAGUZI OKTOBA 29


Na Michael Abel, Shinyanga

Jumuiya ya Maridhiano ya Mkoa wa Shinyanga imewasihi wananchi kujitokeza kwa wingi kupiga kura ifikapo Oktoba 29 mwaka huu, wakisisitiza kuwa ni wajibu wa kila Mtanzania kutimiza haki ya kikatiba ya kuchagua viongozi bora watakaowaletea maendeleo kuanzia ngazi ya kata.

Tamko hilo limetolewa leo Oktaba 18, 2025 na Jumuiya ya Maridhiano ya Mkoa wa Shinyanga inayojumuisha viongozi wa dini zote, viongozi wa kimila pamoja na wadau wa amani kutoka wilaya tatu za mkoa huo.

Wakizungumza kwa pamoja, viongozi hao wamesema wataendelea kuunga mkono jitihada za serikali katika kuhamasisha wananchi kushiriki uchaguzi kwa amani na utulivu, huku wakibainisha kuwa uchaguzi ni tukio muhimu linalopaswa kuendeshwa kwa upendo, mshikamano na heshima kwa kila mtu bila migawanyiko ya kisiasa.

Akisoma tamko la viongozi hao, Makamu Mwenyekiti wa Jumuiya ya Maridhiano Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni Askofu Mstaafu wa Kanisa la KKKT, Emmanuel Makala, amesema kila Mtanzania ana jukumu la kulinda amani, kwani amani ndiyo tunu na msingi wa maendeleo.

“Bila amani hakuna maendeleo. Ni wajibu wa kila raia kuhakikisha nchi inabaki salama kabla, wakati na baada ya uchaguzi,” amesema Askofu Makala.

Kwa upande wake, Aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu, amewasihi viongozi wa dini, machifu na wazee wa mila kuendelea kuliombea taifa katika kipindi hiki cha kuelekea uchaguzi, ili Mungu aendelee kulibariki na kuliongoza Tanzania katika umoja na utulivu.

Naye Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita, amewahakikishia wananchi kuwa maandalizi ya uchaguzi yamekamilika na kwamba siku ya kupiga kura itakuwa salama, huku vyombo vya ulinzi na usalama vikiwa tayari kuhakikisha kila mwananchi anatekeleza haki yake ya kidemokrasia bila hofu.

“Vyombo vya ulinzi na usalama pamoja na tume huru ya uchaguzi vimejipanga kuhakikisha kila mmoja anapiga kura kwa amani na utulivu, na kutimiza haki yake ya msingi iliyowekwa kwa mujibu wa katiba. Tujitokeze kwa wingi, tuwe watulivu na tuheshimu sheria,” amesema Mhita.

Viongozi hao wa dini wamehitimisha kwa kutoa wito wa kudumisha umoja, uvumilivu na maombi kwa taifa, wakisisitiza kuwa amani ndiyo silaha kubwa ya kulinda maendeleo yaliyopatikana nchini.





Kamati ya maridhiano mkoa wa Shinyanga ikitoa tamko hilo.








Mkuu wa Mkoa wa Shinyanga, Mboni Mhita akizungumza kwenye kikao hicho.


Aliyekuwa Waziri wa Maliasili na Utalii nchini, Lazaro Nyalandu, akizungumza wakati wa kikao hicho.




Makamu Mwenyekiti wa Kamati ya Maridhiano na Amani Mkoa wa Shinyanga, ambaye pia ni Askofu Mstaafu wa Kanisa la KKKT, Emmanuel Makala, akizungumza kwenye kikao hicho.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com