Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

HALMASHAURI YA WILAYA YA KISHAPU IMEPOKEA VIFAA VYA RUZUKU VYA UTAMBUZI NA CHANJO YA MIFUGO


Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu,Afisa Mifugo Geofrey Magembe(kulia) akipokea vifaa vya utambuzi na chanzo ya mifugo kutoka kampuni ya uzalishaji na usambazaji wa vifaa na chanjo za mifugo nchini S&J Samwel Raulent (kushoto) Juni 17,2025

Na Sumai Salum-Kishapu

Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga imepokea maboksi ya heleni na chanjo za mifugo kwa awamu ya kwanza Juni 17,2025 kutoka kwenye kampuni ya wazalishaji na wasambazaji wa vifaa vya utambuzi na chanjo ya mifugo S&J.

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji,Afisa Mifugo wa Halmashauri hiyo Geofrey Magembe amesema wamepokea chanjo na heleni za Ng'ombe 30,000 na heleni za Mbuzi na Kondoo 30,000  kwa ajili ya utambuzi wa mifugo Wilayani humo.

"Ni mpango wa serikali ya Awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassani kuhakikisha inatokomeza magonjwa ya mifugo na ndio maana Leo hii Halmashauri tayari tumepokea  chanjo ya Ng'ombe,Mbuzi, Kondoo na kuku wa kienyeji" Amesema Magembe

Magembe ameongeza kuwa heleni hizo zitaisaidia Wizara na serikali kwa ujumla kupata kanzidata halisi ya mifugo iliyoko nchini na kila Wilaya itakuwa na kanzidata sahihi.

"Mfumo huu wa utambuzi kidigitali utakaotumia heleni za kielektroniki utapunguza wizi wa mifugo, utawawezesha wafugaji kupata bima na mikopo na Serikali kufanya tafiti mbalimbali za mifugo na kuweka miundombinu ya ufugaji inayoendana na idadi sahihi ya mifugo iliyopo" ameongeza Magembe.

Ametoa wito kwa wafugaji pindi zoezi hilo la ugawaji litakapoanza baada ya kupokea mwongozo kutoka serikalini kujitokeza kwa wingi kupokea vifaa hivyo vya ruzuku.

Msambazaji kutoka kampuni ya S&J ambao ni wazalishaji na wasambazaji Samwel Raulent  amesema wamekabidhi vifaa hivyo kwa mujubu wa mwongozo wa Wizara katika zoezi zima la utambuzi na bado wanaendelea na uzalishaji na usambazaji zaidi kadri ya maelekezo ya wizara.

Ikumbukwe kuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Samia Suluhu Hassan alizindua chanzo na heleni za mifugo Juni 16,2025 kwa fedha za ruzuku Shilingi Bil.216 katika viwanja vya Nyakabindi Wilayani Bariadi Mkoani Simiyu ikujumuisha vishikwambi 4500 vyenye thamani ya Tsh.Bilion 2.7 vitakavyotolewa kwa maafisa mifugo nchini kote kwa ajili ya kuskani misimbo iliyopo kwenye heleni hizo.

Kupitia kampeni hiyo Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe.Dkt Ashatu Kijaju amemsema chanjo hiyo itatibu magonjwa 5 homa ya mapafu(Ng'ombe),Sotoka(Mbuzi na Kondoo) na Kideri/Mdondo,Ndui na Mafua ya Kuku kwa upande wa kuku za kienyeji huku wakitaraji kuzalisha ajira za muda mfupi 3540 zikihusisha wataalam wa afya ya Mifugo waliopo nje ya mfumo rasmi wa ajira.

Vifaa vya utambuzi wa mifugo heleni za kielektroniki  na chanjo za mifugo vilivyopokelewa na Halmashauri ya Wilaya ya Kishapu Mkoani Shinyanga kutoka kampuni ya uzalishaji na usambazaji S&J Juni 17,2025

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com