ZAIDI YA TANI 200,000 ZA KOROSHO ZASAFIRISHWA KUPITIA BANDARI YA MTWARA MSIMU WA 2023/2024.

 Zaidi ya tani 200,000 (laki mbili) za korosho ghafi, zimesafirishwa kupitia Bandari ya Mtwara katika msimu wa mwaka 2023/2024. 

Akizungumza tarehe 16 Aprili, 2024 kwenye mkutano wa Wadau wa maendeo wa ushoroba wa Mtwara uliofanyika mjini Mtwara, Naibu Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Bandari Tanzania ( TPA) Mhandisi Juma Kijavara amesema mafanikio hayo ni utekelezaji wa agizo la Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. Samia Suluhu Hassan, alilolitoa mwezi Septemba mwaka 2023.

Amesema Korosho ghafi kutoka Mtwara zilikuwa zinasafirishwa kupitia Bandari ya Dar es Salaam lakini kuanzia msimu wa 2023/2024, Korosho zimekuwa zinapitia Bandari ya Mtwara ikiwa pia ni baada ya uwekezaji mkubwa uliofanywa na Serikali katika Bandari hiyo ikiwemo kuongeza vifaa vya kisasa zikiwemo mashine za kupakia na kupakua mizigo na kuongeza idadi ya Wafanyakazi katika Bandari hiyo.

Kuhusu Ujenzi wa Bandari maalumu kwa mzigo mchafu ya Kisiwa Mgao, Mhandisi Kijavara amesema Mkandarasi wa ujenzi wa Bandari hiyo ameshapatikana na kwamba ujenzi unatarajia kuanza Mwezi Mei 2024, na utatekelezwa kwa miezi 24.

Akifungua mkutano huo kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Mkurugenzi wa ufuatiliaji na tathmini Bi. Devotha Gabriel, amesema ushoroba wa Mtwara ni lango kuu la biashara na uwekezaji kwa ukanda wa kusini na Tanzania kwa ujumla na ukiendelezwa ipasavyo utaleta mabadiliko makubwa katika uchumi wa nchi na kuboresha maisha ya Wananchi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post