MCHENGERWA AISHUKURU ORYX,ASAS KWA MSAADA WA VYAKULA , MITUNGI YA GESI KWA WALIOKUMBWA MAFURIKO RUFIJI


Na Mwandishi Wetu

KAMPUNI ya Oryx Gas kwa kushirikiana na Kampuni ya ASAS wamekabidhi msaada wa vyakula na mitungi ya gesi ya Oryx kuwasaidia waathirika wa mafuriko yaliyotokea Wilaya ya Rufiji Mkoa wa Pwani.

Msaada huo umekabidhiwa leo Aprili 13, 2024 jijini Dar es Salaam kwa Mbunge wa Jimbo la Rufiji ambaye pia ni Waziri wa Nchi, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) Mohamed Mchengerwa kuwasaidia wananchi wilayani humo waliopatwa na mafuriko yaliyosababishwa na mvua zinazoendelea kunyesha.

Akizungumza wakati akipokea msaada huo kwa niaba ya wananchi, Waziri Mchengerwa amezishukuru kampuni hizo kwa kuguswa na janga hilo na kujitolea kuwaunga mkongo wana Rufiji kutokana na changamoto iliyowakumba.

"Niko hapa kwa ajili ya kupokea msaada kama tunavyofahamu hali ya Rufiji kila mmoja wenu anatambua kwamba mwaka huu mafuriko yamekuwa makubwa kupita kiasi, tunayafananisha mafuriko ya mwaka huu na mafuriko yaliyotokea mwaka 1972 na mwaka 1974 ...

"Ambapo Baba wa Taifa (Mwalimu Julius Nyerere) alilazimika yeye na Makamu wa Pili wa Rais wakati huo mzee Rashid Mfaume Kawawa kwenda Rufiji wao kwa pamoja kuzunguka na kutoa pole kwa wananchi.

"Leo tunaashuhudia kwa mwamko wa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan ambaye yeye ni mfariji namba moja katika taifa letu alioutoa kwa siku ya jana alipokuwa kule Arusha lakini taarifa ambazo amekuwa akizitoa kuwataka Watanzania kuwa wamoja na kusaidia wale ambao wana nafasi basi wajitolee kwa ajili ya wenzao,"amesema.

Awali kabla ya kukabidhi msaada huo, Meneja Mauzo wa Oryx Gas Shaban Fundi amesema kwa niaba ya Oryx Energies wanatoa pole kwa waathirika wote wa mafuriko yaliyotokea nchini hususan watu wa Rufiji.

"Kampuni ya Oryx Gas ikishirikiana na wadau wenzetu ASAS tumeamua tuwashike mkono wenzetu wa Rufiji kwa kuwapa msaada wa vyakula na mitungi ya gas ili kusaidia watu waliopo katika makambi ya kutolea misaada ya kibinaadam.

"Tumetoa mchele, unga wa sembe, mafuta ya kupikia yenye thamani ya zaidi ya milioni 52. Zaidi tumetoa mitungi mikunwa 100 na majiko 100, pia tumetoa mitungi midogo 100 yenye thamani ya zaidi ya mili 25.Tunampa pole muheshimiwa Waziri Mchengerwa, Wananchi wa Rufiji na Serikali kwa ujumla,"amesema Fundi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post