SIMBA SC YACHEKELEA KIMATAIFA, YAITUNGUA WYDAD 1-0


Na Emmanuel Mbatilo, Dar es Salaam 

Wekundu wa Msimbazi, Simba SC wamefanikiwa kuondoka na ushindi wa bao 1-0 mbele ya Wydad Cassablanca ya Morocco katika mchezo wa mkondo wa kwanza wa hatua ya Robo Fainali ya Ligi ya Mabingwa barani Afrika (CAF CL). 


Mchezo huo uliopigwa kwenye dimba la Benjamini Mkapa jijini Dar es Salaam imeshuhudiwa kandanda safi kutoka kwa wenyeji Simba SC ambao walitawala mchezo kwa muda mwingi na kufanikiwa kupata bao la kuongoza kwenye dakika ya 30’ kupitia kwa Mshambuliaji wao raia wa DR Congo, Jean Baleke aliyeunganisha mpira uliopigwa na Mshambuliaji Kibu Dennis.


Mpaka mapumziko Simba SC ilikuwa mbele kwa bao moja ambalo walililinda mpaka dakika 90’ za mwisho wa mchezo huo, wakisubiri mechi ya mkondo wa pili ambao utachezwa kati ya Aprili 28 au 29, 2023 kwenye dimba la Mohammed V nchini Morocco.


Simba SC wana kazi kubwa ya kulinda goli hilo au ushindi huo katika dimba hilo la Mohammed V na kujihakikishia nafasi ya kufuzu hatua ya Nusu Fainali ya Michuano hiyo mikubwa barani Afrika, mshindi wa mchezo huo atakutana dhidi ya mshindi kati ya CR Belouizdad ya Algeria au Mamelodi Sundowns (Masandawana) ya Afrika Kusini.


Kikosi cha Simba SC kilianza na Wachezaji wengi waliocheza mchezo wa watani wa jadi dhidi ya Young Africans, huku golini wakiendelea kuwa na Golikipa namba tatu, Ally Salim baada ya kuumia Golikipa namba moja, Aishi Manula na Beno Kakolanya akiwa benchi kwenye mchezo huo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments