CHUO CHA MZUMBE WABUNI MIFUMO YA KUSAIDIA USALAMA BARABARANI

 


Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa Chuo Kikuu cha Mzumbe Bi.Rose Joseph,akizungumza na waandishi wa habari (hawapo pichani) kwenye banda la Chuo hicho katika Maonesho ya wiki ya ubunifu 2023 yaliyoandaliwa na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia yanayofanyika uwanja wa Jamhuri Dodoma.
Mhadhiri na Mkuu wa Idara ya Sayansi za Komputa, Dk.Moris Daudi, akielezea jinsi wanavyotengeneza bunifu zao katika kuchangia uchumi shindani wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye banda la Chuo hicho katika Maonesho ya wiki ya ubunifu 2023 yaliyoandaliwa na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia yanayofanyika uwanja wa Jamhuri Dodoma.
Wanafunzi mbalimbali wakipata maelezo kwenye banda la Chuo Kikuu cha Mzumbe katika Maonesho ya wiki ya ubunifu 2023 yaliyoandaliwa na Wizara ya Elimu,Sayansi na Teknolojia yanayofanyika uwanja wa Jamhuri Dodoma.


Na Alex Sonna-DODOMA

WANAFUNZI wa Chuo Kikuu cha Mzumbe wamebuni mifumo mbalimbali ya kiteknolojia itakayolisaidia taifa katika usalama barabarani.

Mifumo mingine ni kusaidia utoaji huduma kwa madaktari wanaozunguka kwenye wodi na namna ya kumlinda mtoto asitoke mbali na nyumbani.

Akizungumza kwenye banda la Chuo Kikuu cha Mzumbe kwenye maonesho ya wiki ya ubunifu inayofanyika uwanja wa jamhuri Dodoma, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Masoko wa chou hicho,Bi. Rose Joseph, amesema bunifu hizo zitaleta chachu na kuchangia uchumi wa taifa.

Amesema maonesho hayo yamekuwa chachu ya kuonesha vipaji na kubaini na kuimarisha mafunzo kwa vitendo kwa wanafunzi wanaosoma masuala ya sayansi na teknolojia.

“Chuo cha Mzumbe kimebobea katika Nyanja mbalimbali lakini mojawapo ni sayansi na teknolojia na kila mwaka tunazalisha vijana ambao wamebobea masuala ya teknolojia, uhandisi na mengine, hii ni fursa ya vijana kuonesha bunifu zao zinazotatua changamoto za taifa,”amesema.Bi.Rose

Naye, Mhadhiri na Mkuu wa Idara ya Sayansi za Komputa, Dk.Moris Daudi, amesema wamekuwa wakishirikiana na wanafunzi kuwajenga kuwa wabunifu ili bunifu zao kuchangia uchumi shindani.

Amebainisha kuwa mfumo wa usalama barabarani ni pale magari yanapoharibika barabarani na madereva kusimamisha pembeni kutengeneza yamekuwa yakisababisha ajali hivyo mfumo huo unalenga kumpa taarifa dereva anayekuja kuwa eneo fulani gari limeharibika ili achukue tahadhali.

“Tunaongezea pia uwezo mfumo kuna baadhi ya matuta yanayowekwa barabarani huwa hayana alama hivyo tunamuongezea uwezo dereva anapokuja aone vizuri, kwa kutumia simu yake,”amesema Dkt.Daudi

Kuhusu mfumo wa kumsaidia daktari kuhudumia wagonjwa wodini, Dk.Daudi amesema mfumo unawezesha kuwekwa kifaa maalum kwenye kitanda cha mgonjwa ili daktari asisumbuke kutembea na karatasi na kujua taarifa za madaktari waliopita kwa mgonjwa.

“Bunifu ya tatu inahusu namna ya kutafuta mtoto, mtoto kuna kifaa anavalishwa kinakuwa ni kidogo mzazi au mwangalizi nyumbani anabaki na simu pale, yule mtoto akitoka mbali zaidi kinampa alarm inakuwa rahisi kumfuata na kumrudisha,”amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments