SERIKALI YAAHIDI KUZIHAKIKI UPYA HOTELI ZA KITALII


***************************

Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja ameiambia Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi Maliasili na Utalii kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii itayafanyia kazi maelekezo yaliyotolewa na kamati hiyo kuhusu kuzifanyia upya uhakiki hoteli na loji za kitalii ambazo hazifanyi kazi vizuri ili kukabiliana na changamoto ya huduma za malazi kwa watalii hapa nchini.

Mhe. Mary Masanja ameyasema hayo kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii leo jijini Dodoma mara baada ya kupokea maoni, ushauri na maelekezo yaliyotolewa na Kamati ya Kudumu ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu taarifa ya Wizara ya Utendaji kazi wa Hoteli na Loji za kitalii za Serikali zilizobinafsishwa.

Amesema Tanzania imekua ikipokea watalii wengi hali iliyosababisha kuongezeka kwa mahitaji ya huduma za malazi kwa watalii kufuatia kazi kubwa iliyofanywa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan ya kutangaza vivutio vya utalii kupitia Filamu ya Royal Tour.

“Namshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kuzindua filamu ya Royal Tour ambayo kwa sasa matunda yake yanaonekana kwa kuongezeka kwa mahitaji ya huduma za malazi kwa watalii hapa nchini” amebainisha Mhe. Masanja.

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii, Mhe. Ally Juma Makoa ameeleza kuwa Wizara ya Maliasili na Utalii inapaswa kufanya maamuzi kwa kufuata sheria zilizopo ili hoteli na loji ambazo hazifanyi kazi ziweze kutoa huduma ili kwenda na kasi ya idadi ya watalii pia kuongeza mapato yatokanayo na biashara za utalii, kuongeza tija na ufanisi katika uendeshaji wa hoteli za kitalii.

“Inabidi tufanye maamuzi ya haraka sana ya kuona namna gani tunaweza kuboresha huduma za hoteli na loji ambazo hazifanyi kazi ili kuendana na kasi ya idadi ya watalii wanaokuja nchini baada ya kuzinduliwa kwa Royal Tour” amesisitiza Mhe. Makoa.

Awali akiwasilisha taarifa ya hali ya loji na hoteli za kitalii Afisa Usimamizi wa Fedha Mkuu kutoka Ofisi ya Msajili wa Hazina Thabiti Dokodoko amesema uwekezaji katika hoteli na loji umeisaidia Serikali kuingiza kiasi cha shilingi bilioni 60.38 kwa kipindi cha miaka mitano (2018/19-Desemba,2022).

Ameongeza kuwa uwekezaji katika hoteli na loji za kitalii unalenga katika kutatua changamoto ya huduma za malazi hususan idadi ya vyumba na vitanda.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments