PURA YATOA MSAADA KWA WAGONJWA WA SARATANI OCEAN ROAD


Mkurugenzi Mkuu wa PURA Mhe. Charles Sangweni (kushoto) akikabidhi vifaa hivyo kwa Muuguzi Kiongozi wa Taasisi ya Saratani ya Ocean Road, Bi. Chausiku Chapchap. Tukio hilo limefanyika siku ya leo tarehe 30 Januari, 2023 Jijini Dar es Salaam.

***********************

Mamlaka ya Udhibiti Mkondo wa Juu wa Petroli (PURA) leo, Januari 30, 2023 imetoa msaada wa vifaa mbalimbali vya kujikimu kwa wagonjwa wa saratani wanaopatiwa matibabu katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road (ORCI).

Msaada huo umehusisha vifaa kama sabuni za kufulia na kuogea, miswaki na dawa za meno, sukari, toilet paper pamoja na tissue.

Akizungumza baada ya kukabidhi vifaa hivyo, Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Mha. Charles Sangweni amesema Mamlaka hiyo imeamua kutoa msaada wa vifaa hivyo ili kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuimarisha huduma za afya nchini ikiwa ni pamoja na kuboresha mazingira ya hospitali na vituo vya afya.

“Sisi ni taasisi ya Umma yenye wafanyakazi Watanzania ambao kwa njia moja au nyingine wagonjwa wa saratani ni ndugu na jamaa zetu hivyo tumeona ni muhimu kuendeleza utamaduni wa kujitoa kwa jamii, na kusaidia Watanzania wenzetu ambao wanakabiliwa na maradhi ya saratani,” aliongeza.

Naye Muuguzi Kiongozi wa taasisi hiyo Bi Chausiku Chapchap ameishukuru PURA kwa msaada walioutoa na kueleza kuwa utasaidia zaidi wagonjwa ambao hawana ndugu jijini Dar es Salaam hivyo kushindwa kuwaletea vifaa hivyo mara kwa mara.

“Matibabu ya wagonjwa ya saratani huchukua muda mrefu na wagonjwa wengi hutokea nje ya mkoa hivyo vifaa hivi vitawasaidia kujikimu katika matumizi ya kila siku,” alieleza.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments