NYUMBA ZA WATUMISHI WA KITUO CHA AFYA NYABILEZI ZIMEJENGWA NA TASAF KUWAWEZESHA WATUMISHI KUTOA HUDUMA BORA KWA WANANCHI


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akizungumza na wananchi na walengwa wa TASAF wa Kijiji cha Nyabilezi katika kituo cha Afya cha Nyabilezi (Nyabilezi Health Centre) wilayani Chato wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini mkoani Geita.

Sehemu ya wananchi na Walengwa wa TASAF wa Kijiji cha Nyabilezi wakimsikiliza Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi (hayupo pichani) mara baada ya Naibu Waziri huyo kukitembelea kituo cha afya Nyabilezi wilayani Chato wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini mkoani Geita.


Katibu Tawala Mkoa wa Geita, Prof. Godius Kahyarara akimshukuru Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi kwa kufanya ziara ya kikazi yenye lengo la kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini mkoani Geita.


Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi akielekea kukagua ujenzi wa nyumba za watumishi katika kituo cha afya cha Nyabilezi (Nyabilezi Health Centre) kilichopo wilayani Chato wakati wa ziara yake ya kikazi ya kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini mkoani Geita, wengine ni watendaji wa mkoa huo.


Mganga Mfawidhi wa kituo cha afya cha Nyabilezi (Nyabilezi Health Centre) Bi. Lucia Simbila (Wa kwanza kulia) akifafanua jambo kuhusu utendaji kazi wa kituo hicho kwa Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi wakati wa ziara ya kikazi ya Naibu Waziri huyo iliyolenga kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini wilayani Chato mkoani Geita.


Mwonekano wa nyumba za watumishi zinazojengwa katika Kituo cha Afya cha Nyabilezi (Nyabilezi Health Centre) kwa ufadhili wa OPEC kupitia uratibu TASAF.

****************************

Na. Veronica Mwafisi - Chato

Tarehe 26 Januari, 2023



Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Deogratius Ndejembi amesema Serikali ya Awamu ya Sita kupitia mradi wa TASAF imejenga kituo cha afya cha Nyabilezi (Nyabilezi Health Centre) pamoja na nyumba za watumishi zinazoendelea kujengwa ili kuwawezesha watumishi wa kituo hicho cha afya kuwa na makazi mazuri ya kuishi yatakayowawezesha kutoa huduma bora na ya haraka kwa wananchi wa Kijiji cha Nyabilezi kilichopo katika Halmashauri ya Wilaya ya Chato.

Mhe. Ndejembi amesema hayo, wakati akizungumza na wananchi na walengwa wa TASAF wa kijiji cha Nyabilezi, mara baada ya kukagua Kituo cha Afya cha Nyabilezi na nyumba za watumishi wa kituo hicho, wakati wa ziara yake ya kikazi yenye lengo la kukagua utekelezaji wa Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini mkoani Geita.

“Nimetoka kukagua ujenzi wa nyumba ambazo watakaa watumishi kwa ajili ya kuwahudumia wakazi wa Nyabilezi, hivyo wana Nyabilezi mtegemee kupata huduma bora kutoka kwa watumishi wa kituo chenu cha afya,” Mhe. Ndejembi amesisitiza.

Mhe. Ndejembi amefafanua kuwa, nyumba hizo zinajengwa kupitia mradi wa TASAF, ambao upo chini ya usimamizi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan amedhamiria kuboresha makazi ya Watumishi wa Umma ili waweze kutoa huduma bora kwa wananchi katika maeneo mbalimbali.

Ili wanachi waendelee kupata huduma katika Kituo cha Afya cha Nyabilezi, Mhe. Ndejembi amewataka wakazi wa Nyabilezi kuendelea kuitunza miundombinu yote iliyopo katika kituo hicho cha afya kwa ajili ya manufaa ya kizazi cha sasa na cha baadae.

Kwa upande wake, Katibu Tawala Mkoa wa Geita, Profesa Godius Kahyarara amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan na wasaidizi wake kwa kuwezesha miradi mingi ya maendeleo na ya kijamii kutekelezwa katika mkoa wa Geita.

Mradi wa ujenzi wa Kituo cha Afya cha Nyabilezi pamoja na nyumba za watumishi wa kituo hicho ambazo zinazoendelea kujengwa, unaratibiwa na Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF) kupitia ufadhili wa OPEC.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments