HIZI NDIYO NCHI AMBAZO NI VIGUMU KWA MWANAUME KUPATA MKE WA KUOA


JAPOKUWA inafahamika kwamba, katika jumla ya idadi ya watu bilioni 7. 5 waliopo dunia leo hii, idadi ya wanaume na wanawake inapishana kwa kiasi kidogo, zipo baadhi ya nchi ambazo wanaume ni wengi kuliko wanawake, kiasi kwamba inakuwa kazi ngumu kwelikweli kumpata mwanamke wa kuoa.

SWEDEN

Nchini Sweden, inaelezwa kwamba idadi ya wanaume, inazidi kwa 12,000 zaidi ya idadi ya wanawake waliopo na kundi kubwa ni la vijana. Idadi hii inatarajiwa kuongezeka zaidi kwa hiyo, wanaume wengi wanajikuta katika wakati mgumu wa kupata wachumba wa kuingia nao kwenye ndoa.



Sababu nyingine inatajwa kwamba ni ongezeko la wahamiaji kutoka kwenye nchi zenye vita ambao wanapata hifadhi kwenye nchi hiyo na baadaye kupewa uraia. Ongezeko la wahamiaji, limesababisha wananchi wengi wa Sweden wasiotaka shida, kuhamia kwenye nchi nyingine zisizo na idadi kubwa ya wahamiaji na wengi wanaoondoka, ni wasichana.

AFGHANISTAN

Kabla ya nchi ya Afghanstan kukumbwa na vita, ilikuwa ikisifika kwa kuwa na wanawake wengi warembo waliokuwa wakionekana kwa wingi mitaani, hasa katika Jiji la Kabul.



Hata hivyo, tangu machafuko yaikumbe nchi hiyo, idadi ya wanawake imepungua sana, sababu kubwa ni kwamba wanawake wengi na watoto wameikimbia nchi kutokana na vita na kwenda kutafuta hifadhi katika nchi zenye usalama. Waliobaki ni wanaume wanaoendelea kupambana na machafuko ya mara kwa mara yanayoibuka na kupotea, matokeo yake imekuwa vigumu sana kupata mke wa kuoa.

NIGERIA

Nchini Nigeria, uwiano kati ya wanawake na wanaume, haupo sawa. Wanaume ni wengi kuliko wanawake na sababu kubwa, inatajwa kwamba wanawake wa Kinigeria, wamekuwa wakiikimbia nchi yao na kwenda kutafuta hifadhi kwenye mataifa mengine kutokana na sababu mbalimbali, zikiwemo kukimbia ndoa za utotoni, tohara za wanawake na hali ngumu ya kimaisha.



Hivi karibuni, serikali ya nchi hiyo ilieleza kuhusu tatizo la vijana wengi waliofikia umri wa kuoa, kukosa wanawake wa kuwaoa.

UGIRIKI

Kwa kipindi kirefu, nchi ya Ugiriki ilikuwa ikitumika kama kituo cha watu wanaotoka Ulaya, hasa katika nchi za Uingereza na Ufaransa kwenda kwenye mabara mengine. Kutokanana uzuri wa hali ya hewa ya Ugiriki pamoja na mandhari yake, wasafiri wengi wakawa wanavutiwa kuendelea kukaa kwenye nchi hiyo na baadaye, idadi ya wahamiaji kutoka kwenye mataifa makubwa ya Ulaya iliongezeka na wengi kati yao, walikuwa ni wanaume.



Hali imeendelea hivyo kwa miaka mingi na kusababisha idadi ya wanawake kutotosheleza idadi ya wanaume wanaozidi kuongezeka kila kukicha. Hivi sasa ni vigumu sana kupata mke wa kuoa nchini Ugiriki.

MISRI

Misri ni moja ya nchi yenye idadi kubwa ya watu kwenye nchi za Kiarabu na barani Afrika. Kama zilivyo nchi nyingine za Kiarabu, wanawake wanatakiwa kufanya shughuli za nyumbani tu na kutoonekana hovyo mitaani.



Wengi wameitumia fursa hii kujiendelea kielimu wakiwa majumbani na wanawake wengi wa Misri, ni wasomi wenye digrii kadhaa, walizozipata kwa kujiendeleza wakiwa majumbani mwao na baadaye kwenda vyuo vikuu.



Hali hiyo imesababisha wanawake wengi wasomi, kuanza kutafuta ajira nje ya nchi, ambako wanawake wana uhuru zaidi na tayari wengi wameondoka na kwenda kufanya kazi mbalimbali kulingana na elimu zao, hali iliyosababisha wanaume wengi wapate kazi kwelikweli wanaposaka wanawake wa kuwaoa.

CHINA

China ndiyo nchi yenye watu wengi kuliko wote duniani, lakini katika idadi ya watu wote nchini humo, wanaume wanawazidi wanawake kwa idadi ya watu milioni 40. Tofauti hii kubwa kati ya idadi ya wanawake na wanaume, imesababishwa na Wachina kuwa na kawaida ya kuchagua watoto, na mwanamke anapokuwa na ujauzito wa mtoto wa kike, hulazimishwa kutoa ujauzito huo kwani Wachina wengi wanaamini kwamba mtoto wa kiume ndiyo mwenye thamani katika jamii.



Hali hiyo imesababisha uhaba mkubwa wa wanawake mitaani, kiasi cha serikali kuingilia kati na sasa, vijana wa kiume kutoka China wanaruhusiwa kwenda kutafuta wanawake nchini Urusi, ambako kuna uhaba wa wanaume.

MAREKANI

Yawezekana ukashangazwa na kusikia kwamba nchini Marekani nako kuna uhaba mkubwa wa wanawake. Ukweli ni kwamba, katika baadhi ya majimbo, idadi ya wanawake ni ndogo kuliko wanaume.



Kwa mfano, katika majiji ya Los Angeles na Las Vegas, idadi ya wanawake ni ndogo kuliko wanaume kwa wastani wa wanaume 157 kwa wanawake 151, hali inayofanya iwe vigumu kupata wasichana wazuri wa kuoa.

INDIA

India ni miongoni mwa nchi zenye watu wengi zaidi duniani na inatarajiwa kwamba ifikapo 2024, itaizidi China. Licha ya idadi hiyo kubwa ya watu, India ina uhaba mkubwa wa wanawake kutokana na mila potofu ya nchi hiyo kwamba watoto wa kiume wana umuhimu sana kuliko wa kike wakiamini kwamba wana msaada mkubwa sana katika familia pale wanapofikia umri wa kujitegemea.



Wanaume wanawazidi wanawake kwa idadi ya watu milioni 37, hali inayofanya iwe vigumu sana kupata mke wa kuoa.

FALME ZA KIARABU

Katika kipindi cha karne ya 20 falme za kiarabu zilikuwa na idadi ya watu 40,000 tu, Kati ya hao wanawake wakiwa ni 22,000.Hata hivyo ugunduzi wa mafuta umesababisha nchi hiyo ibadilike haraka na wahamiaji wengi kutoka nchi mbalimbali,wengi wakiwa ni wanaume ambao wamejazana nchini humo,kutafuta maisha.



Hali hiyo imesababisha kuwe na uhaba mkubwa wa wanawake jambo linalowapa shida wanaume wanapofikia umri wa kuoa.

QATAR

Nchi ya Qatar ni miongoni mwa nchi zenye utajiri mkubwa wa mafuta lakini kijiografia ina eneo dogo na wananchi wazawa wachache. Hata hivyo kutokana na utajiri wa mafuta imepiga hatua kubwa ya kimaendeleo, hali ambayo imesababisha wahamiaji wengi kukimbilia na kutafuta maisha.



Matokeo yake wanaume wamekuwa wengi kwa wastani wa 3:1, katika kila watu wa 4 wa 3 ni wanaume na mmoja ni mwanamke na kuifanya kuwa nchi yenye wanawake wachache zaidi duniani.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments