KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA BAJETI YAIPONGEZA WIZARA YA MALIASILI NA UTALII KWA MATUMIZI MAZURI YA FEDHA ZA UMMA


Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Daniel Sillo akizungumza na wananchi wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti katika Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma

Katibu Mkuu, Wizara ya Maliasili na Utalii, Prof. Eliamani Sedoyeka akiishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti baada ya ziara ya kukagua miradi ya ujenzi wa lango la kuingilia wageni, barabara ya kilomita 47.2 na ujenzi wa Picnic Site. kwenye Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma.Afisa Uhifadhi Miundombinu wa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA), Noti Mgaya akitoa maelezo kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu ujenzi wa Picnic Site katika Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani DodomaNaibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) akitoa ufafanuzi kwa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti kuhusu mradi wa ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 47.2 katika Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti ikikagua mradi wa ujenzi wa barabara yenye urefu wa kilomita 47.2 katika Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma.

*************

Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, Mhe. Daniel Sillo ameipongeza Wizara ya Maliasili na Utalii kwa matumizi mazuri ya fedha za umma katika utekelezaji wa miradi ya ujenzi wa lango la kuingilia wageni, barabara ya kilomita 47.2 na ujenzi wa Picnic Site. kwenye Pori la Akiba Mkungunero.

Ameyasema hayo leo wakati wa ziara ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti ya kukagua utekelezaji wa miradi mbalimbali kwenye Pori la Akiba Mkungunero lililopo Wilaya ya Kondoa Mkoani Dodoma.

“Tuipongeze Wizara ya Maliasili na Utalii kwa usimamizi mzuri wa fedha hizi za umma ambazo zinaleta tija katika suala zima la maliasili na utalii hapa nchini” Mhe. Sillo amesisitiza.

Amesema Wizara ya Maliasili na Utalii ilipata kiasi cha shilingi bilioni 90.2 ambapo bilioni 12.9 ilikabidhiwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) na kisha kiasi cha shilingi milioni 672 kupelekwa Pori la Akiba la Mkungunero kwa ajili ya kuboresha eneo hilo ili kuvutia wawekezaji na watalii.

Amefafanua kuwa uboreshaji wa miundombinu ya Pori ya Akiba la Mkungunero utafungua fursa za utalii nchini Tanzania na pia itaongeza uchangiaji wa Sekta ya Maliasili na Utalii kwenye pato la Taifa ambapo kwa sasa sekta hiyo inachangia takribani asilimia 17 ya pato la Taifa na asilimia 25 ya fedha za kigeni.

Naye, Naibu Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mary Masanja (Mb) Wizara ya Maliasili na Utalii ilifaidika na mgao wa fedha za Mpango wa Maendeleo kwa Ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO-19 ambapo ilipokea kiasi cha shilingi bilioni 88.57 sawa na asilimia 98 ya mpango huo.

Amefafanua kuwa Pori la Akiba Mkungunero ilitengewa kiasi cha shilingi milioni 672 na mpaka sasa fedha hizo zimepokelewa zote na zimepangwa kutekeleza miradi mitatu ambayo ni ujenzi wa lango la kuingilia wageni, barabara ya kilomita 47.2 na ujenzi wa Picnic Site.

Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti iko Wilayani Bababti na inaendelea na ziara ya kukagua miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wizara ya Maliasili na Utalii.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments