KKAM LAWASIMIKA WATUMISHI WAWILI, DR. LANGAS MOLEL NA DR. OLAIS MONABAN


Msaidizi wa Askofu Dr Philemon Olaisi Molel (MONABAN) akiwa anavalishwa rasmi vazi la kuwa Askofu msaidizi wa kanisa la kilutheri Afrika Mashariki jimbo la Arusha Mashariki.


Na Rose Jackson - Arusha

Kanisa la kilutheri Afrika Mashariki (KKAM) limewasimika na kuwaingiza kazini watumishi wawili amabo ni mchungaji Dr. Philemon Langas Molel kuwa Askofu wa Jimbo la Arusha Mashariki pamoja na mchungaji Dr. Philemon Olaisi Molel (MONABAN) kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo Hilo .


Askofu mkuu wa kanisa hilo Askofu Osca John Olotu akizungumza katika ibada ya kuwasimika watumishi hao iliyofanyika maeneo ya Ngulelo ,amesema kuwa wametimiza agizo la Mungu aliloagiza la enendeni ulimwenguni mkahubiri Injili.


Amesema kuwa ili kusudi hilo litimie lazima wahubiri Injili kupitia utumishi waliopewa hivyo kupitia watumishi hao wanatarajia waumini kuongezeka na wanatarajia kufikia vijiji vyote ili kupeleka Injili.

Ameongeza kuwa wao hawatafanya mashindano ya aina yeyote badala yake watasimamia kusudi moja la kuhubiri Injili ya Yesu Kristo.

Akizungumza Mara baada ya kuingizwa rasmi kazini Askofu Dr Philemon Langas Molel amesema kuwa anamshukuru Mungu kwa daraja jipya alilolipokea na wajibu walio nao ni kuhakikisha wanaotesha makanisa sehemu mbali mbali.


Ameongeza kuwa kanisa hilo na mengine hayana tofauti kwani yote yanalenga kumhubiri Yesu Kristo lakini tofauti ndogo ikiwa ni kutowabariki wanawake kuwa wachungaji.


Kwa upande wake msaidizi wa Askofu mchungaji Dr. Philemon Olaisi Molel (MONABAN) akiongea mara baada ya kubarikiwa na kuingizwa kazini amesema kuwa amesikia furaha kwani kanisa hilo linahubiri amani na ushirikiano

'Kanisa letu tutakuwa tunahubiri upendo, amani, ushirikiano na umoja katika maeneo yote nchini na hata kwenye nchi za jumuiya ya Afrika Mashariki", ameisisitizia Monaban


Monaban amedai kuwa kwa kuwa Mungu amempa vipawa viwili ikiwemo cha Siasa pamoja na utumishi wa madhabuni atavitumia vyote kwa pamoja kwa kuwa atawahidumia watu wake kiroho na kimwili na atahakikisha anavitumia vizuri kama Mungu alivyokusudia.


Katibu wa kanisa hilo Afrika Mashariki Heroki Mkwizu amesema kuwa parokia nyingi kwa sasa zitafunguliwa Arusha pamoja na maeneo mengine mara baada ya kuongezeka kwa watumishi hao.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments