CWT BAGAMOYO YAGAWA MAJIKO YA GESI KWA WALIMU SHULE ZA MSINGI NA SEKONDARI

Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kisanga ,Juma Ibrahimu akipokea jiko la gesi kutoka kwa viongozi wa CWT wilaya ya Bagamoyo


Na Elisante  Kindulu - Bagamoyo
CHAMA Cha Walimu Wilaya ya BAGAMOYO (CWT) kimetoa majiko ya gesi kwenye baadhi ya shule za Msingi na Sekondari katika Wilaya hiyo yenye halmashauri mbili za Bagamoyo na Chalinze mwishoni mwa wiki.

Katibu wa Chama Cha Walimu Wilaya ya Bagamoyo Bw. Shaaban Tessua aliyataja malego ya kutoa majiko hayo kuwa ni kuwarahisishia walimu kupata huduma ya CHAKULA kwa urahisi bila kupoteza muda wa vipindi darasani, Kusaidia kuendesha mijadala ya pamoja wawapo katika mkusanyiko wa kupata huduma ya chakula pamoja na kujenga upendo , mshikamano na ushirikiano.

Bw. Tessua  alizitaja shule zilizonufaika na mgawo huo kuwa ni shule ya Sekondari Talawanda, shule ya Msingi Talawanda, Vundumu ,  Kisanga, Msanga, Msigi, Ludiga, Kisambi na Shule ya Msingi Mindukene ambazo zote zipo katika halmashauri ya Chalinze.

Kwa upande wa halmashauri ya Bagamoyo shule zilizonufaika  ni pamoja na Shule ya msingi Ukuni, shule ya msingi Mwanamakuka na shule ya msingi Mbaruku.

Bw. Tessua alisema zoezi hilo ni endelevu na lengo ni kuzifikia shule zote katika Wilaya hiyo. 

Mbali na kutoa majiko hayo mashuleni , viongozi wa Chama hicho kwa kushirikiana na Kaimu Katibu wa Tume ya huduma kwa walimu(TSC) wilayani humo walizungumza na walimu juu haki na wajibu wao mahala pa kazi pamoja na kusajiri wanachama wapya.

Katika ziara hizo Katibu aliongozana na Kaimu Katibu wa TSC Wilaya ya Bagamoyo ,Bw. Titus Ndomba, Mwenyekiti wa CWT Bagamoyo, Mwl. Hamisi Kimeza, Mweka Hazina wa CWT wilayani humo Siza Mnjokava, 

Mwakilishi wa walimu wenye mahitaji Maalum Mwl. Phinus Tuarira, Mwakilishi wa walimu Vijana , Mwl. David  Phares na Mjumbe wa Kamati ya utendaji , Mwl. Beo Sumari.

Wengine Ni Mwl. Anna Choaji( Katibu kitengo Cha walimu wanawake), Mwl. Theresia Kilimo( Mweka Hazina kitengo Cha Walimu wanawake), Pili Mrope (Mjumbe ), Selestine Cassian(Mjumbe) na Teddy Setebe (Mjumbe).

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments