MWANZA KUANZA ZOEZI LA KUWAONDOA WATOTO MITAANI ..KIVULINI YASHAURI MBINU RAFIKI ZITUMIKE

Serikali mkoani Mwanza inatarajia kuanza zoezi la kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani ambao wamekithiri hususani katika Jiji la Mwanza na kuhakikisha watoto hao wanarejea katika familia zao na kupata haki yao ya msingi ya kurejea shule.

Hayo yameelezwa Aprili 08, 2022 kwenye kikao kazi cha Kamati ya Kamati ya Kupambana na Ukatili wa Kijinsia kwa wanawake na watoto (MTAKUWWA) ngazi ya Mkoa Mwanza ambacho kimelenga kujadili na kuweka mikakati ya pamoja ya kuwaondoa watoto mitaani na kutokomeza utoro katika Shule za Msingi na Sekondari mkoani Mwanza.

Akifungua kikao hicho, Katibu Tawala Mkoa Mwanza Ngusa Samike ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo ametaka uwepo mkakati wa kuwaelimisha wazazi na walezi ili wasiwe chanzo cha watoto wao kukimbilia mitaani.

Ameonya kuwa baada ya wazazi na walezi kupata elimu, watakaoshindwa kutoa ushirikiano ili kuhakikisha watoto wao hawakimbilii mitaani hatua kali za kisheria zichukuliwe dhidi yao hatua itakayosaidia kudhibiti wimbi la watoto kukimbia mitaani kiholela.

Samike amebainisha kuwa Serikali ya Rais Samia Sauluhu Hassan imekuwa ikitoa fedha nyingi kwa ajili ya sekta ya elimu ambapo katika kipindi cha miezi mitano iliyopita, Mkoa Mwanza umepokea shilingi bilioni 20.5 hivyo si vyema watoto kukosa haki ya kupata elimu na kukimbilia mitaani.

Naye Afisa Maendeleo Mkoa Mwanza, Isack Ndassa amesema zaidi ya asilimia 90 ya watoto walio mitaani wana umri wa kwenda shule lakini wanakosa haki hiyo ya kupata elimu kutokana na sababu mbalimbali ambazo zinazuilika.

Ameshauri viongozi wanaounda Kamati ya MTAKUWWA wakiwemo Polisi Kata, Watendaji wa Kata, Maafisa Elimu Kata, Maafisa Maendeleo Kata, Maafisa Ustawi wa Jamii Kata na viongozi wa dini kushiriki ipasavyo kwenye zoezi la kuwabaini watoto walioacha shule na kukimbilia mitaani ili kuwarejesha katika familia zao na kwamba zoezi hilo lisimamiwe kwa kuzingatia misiki ya haki za binadamu.

Naye Kaimu Afisa Elimu Mkoa Mwanza, Mwl. Maenda Chambuko amesema katika kipindi cha kuanzia mwezi Januari hadi Aprili mwaka huu 2022 kuna jumla ya wanafunzi watoro 19,133 katika Shule za Msingi na walipo Shule ni 913,335 huku kwa Shule za Sekondari wanafunzi watoro wakiwa ni 7,594 na walio Shule wakiwa ni 222,132. 

Amesema Serikali imeweka mifumo rafiki kwa wanafunzi ambao hawako shuleni kutokana na sabababu mbalombali ikiwemo mimba na utoro kurejea shuleni hivyo jitihada zifanyike ili kuhakikisha kila mtoto anapata haki ya kwenda Shule.

Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la KIVULINI, Yassin Ally ameshauri mbinu rafiki kutumika wakati wa kutekeleza zoezi la kuwaondoa watoto mitaani pamoja na kutokomeza utoro mashuleni akishauri mbinu kama za utoaji uji ama chakula mashuleni kutumika ili kuhamisha watoto kupenda Shule.

Yassin ameshauri pia waalimu kuwa na mbinu rafiki kwa wanafunzi na kuacha tabia ya kuwashughulikia kwa adhabu kali kutokana na kukosa mahitaji ya shule ikiwemo sare ama viatu hatua itakayosaidia kupunguza utoro mashuleni. Pia ameshauri utaratibu wa kuwaondoa shuleni wanafunzi watoro ndani ya siku 90 kwani linakinzana na azma ya Rais Samia Suluhu Hassan kuhamasisha wanafunzi kurejea shule.

Kwa upande wake Mjumbe wa Baraza la Watoto Mkoa Mwanza, Glory Theonest amesema changamoto kubwa ambayo imekuwa ikisababisha utoro kwa wanafunzi hususani wa kike ni tabia ya baadhi ya waalimu kuwataka kingono na wanapokataa wanakuwa wanaadhibiwa vikali hata kwa makosa madogo na kuomba waalimu ambao pia ni walezi na wazazi kuwa marafiki wa wanafunzi na kuwasaidia kimasomo ili kufikia ndoto zao.

Kikao kazi hicho cha MTAKUWWA Mkoa Mwanza ni kikao cha kwanza katika kuweka mikakati ya kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani na kutokomeza utoro mashuleni ambapo vikao zaidi vitafanyika ili kuja na mbinu zitakazosaidia zoezi hilo linalotarajiwa kuanza kati ya mwezi Mei ama Juzi mwaka huu 2022 kufanikiwa.
Na George Binagi-GB Pazzo, BMG
Katibu Tawala Mkoa Mwanza, Ngusa Samike (kushoto) akifungua kikao kazi cha Kamati ya MTAKUWWA Mkoa Mwanza kilicholenga kuweka mikakati ya kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani pamoja na kutokomeza utoto kwa wanafunzi mashuleni Mwenyekiti wa Kamati hiyo ni Katibu Tawala Mkoa Mwanza. Katikati ni Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally na kulia ni Afisa Programu Mwandamizi wa Shirika hilo, Grace Mussa.
Katibu Tawala Mkoa Mwanza, Ngusa Samike akifungua kikao kazi cha Kamati ya MTAKUWWA Mkoa Mwanza kilicholenga kuweka mikakati ya kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani pamoja na kutokomeza utoto kwa wanafunzi mashuleni.
Katibu Tawala Mkoa Mwanza, Ngusa Samike akifungua kikao kazi cha Kamati ya MTAKUWWA Mkoa Mwanza kilicholenga kuweka mikakati ya kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani pamoja na kutokomeza utoto kwa wanafunzi mashuleni.
Afisa Maendeleo Mkoa Mwanza, Issack Ndassa (kushoto) akizungumza kwenye kikao kazi hicho cha MTAKUWWA Mkoa Mwanza kilicholenga kuweka mikakati ya kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani pamoja na kutokomeza utoro mashuleni.
Kaimu Afisa Elimu Mkoa Mwanza, Maenda Chambuko akiwasilisha takwimu za hali ya utoro katika Shule za Msingi na Sekondari mkoani Mwanza.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Kutetea Haki za Watoto na Wanawake KIVULINI, Yassin Ally akizungumza kwenye kikao kazi cha kuweka mikakati ya kuwaondoa watoto wanaoishi mitaani pamoja na kutokomeza utoro katika Shule za Msingi na Sekondari mkoani Mwanza.
Mkurugenzi Mtendaji Shirika la KIVULINI, Yassin Ally akizungumza kwenye kikao hicho.
Wajumbe wa Kamati ya MTAKUWWA Mkoa Mwanza wakifuatilia kikao kazi cha kujadili na kuweka mikakati ya kuondoa watoto wanaoishi mitaani pamoja na kuzuia utoro katika Shule za Msingi na Sekondari mkoani Mwanza.
Wajumbe wa MTAKUWWA Mkoa Mwanza wakiwa kwenye kikao kazi cha kupanga mikakati ya kuwaondoa watoto wanaishi mitaani na kutokomeza utoro mashuleni.
Wajumbe wa Kamati ya MTAKUWWA Mkoa Mwanza wakiwa kwenye kikao kazi hicho.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments