MHASIBU HALMASHAURI YA MASWA AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA UHUJUMU UCHUMI

Na Costantine Mathias, Simiyu.

TAASISI ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU) Wilaya ya Maswa Mkoani Simiyu, imemfikisha Mahakamani Mhasibu msaidizi Idara ya Ushirika katika halmashauri ya Wilaya  hiyo Daud Makoye hiyo kwa makosa ya Uhujumu uchumi.

Ofisa huyo amefikishwa jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi mkoa wa Simiyu na kusomewa Mashtaka mawili yanayomkabili ambayo ni kuchepusha mali ya serikali ikiwa kwa madhumuni yasiyohusiana na ilivyokusudiwa.


Kosa la Pili ni Ubadhirifu na ufujaji wa mali kinyume na kifungu cha 28 cha sheria ya kuzuia na kupambana na Rushwa No. 11 ya Mwaka 2007.


Mbele ya Hakimu mkazi wa Mahakama hiyo Martha Mahumbuga, Mwendesha Mashtaka wa Serikali Josephat Jankila ameelezea Mahakama kuwa Mshtakiwa alitenda makosa hayo tarehe 23/09/2021 huko katika Wilaya ya Maswa.


Mwendesha Mashtaka huyo alisema kuwa Mshtakiwa akiwa mwajiliwa wa halmashauri ya Maswa kama mhasibu msaidizi wa halmashauri idara ya Ushirika alifanya ubadhilifu wa Sh. Milioni tano laki tano na ishirini na nne mia mbili. (5,524,000,200).


Alisema kuwa Ofisa huyo alitumia fedha hizo kwa matumizi yake binafsi wakati akijua kuwa ni mali ya Umma, fedha ambazo zilitolewa na Amcos ya WITAMILYA iliyoko kwenye Wilaya hiyo kwa ajili ya kulipa kodi Tume ya maendeleo ya Ushirika (TCDC) pamoja na Chama Kikuu cha Ushirika Mkoa wa Simiyu (SIMCU).


Aidha katika maelezo ya kosa la pili, Mwendesha Mashtaka huyo alisema kuwa Mshtakiwa alichepusha fedha hizo kwa madhumuni yake binafsi kinyume na kifungu  cha 29 cha sheria ya kuzuia na kupambana na Rushwa No. 11 ya Mwaka 2007.


Mara baada ya kusomewa mashtaka hayo,mshitakiwa alikana makosa yote ambapo hakimu alihaitisha kesi hiyo mpaka mnamo April 24, mwaka huu kwa ajili ya  kusomwa kwa hoja za awali.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments