KATIBU MKUU MADINI ATEMBELEA GEITA GOLD MINING LIMITED (GGML), AIPONGEZA KWA KUZINGATIA SHERIA


Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Adolph Nduguru (kushoto) akipata maelezo kutoka kwa Kaimu Meneja Madini, Gilbert Chamlonde (kulia) kuhusu shimo la wazi la Nyankanga lililokuwa likifanya kazi kati ya mwaka 1990 na 2020.
Makamu wa Rais wa AngloGold Ashanti anayesimamia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo (katikati), akitoa maelezo kwa Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Adolph Nduguru kuhusu shughuli mbalimbali za GGML.
(Kutoka kushoto) Meneja Mwandamizi wa Fedha, Ikingo Gombo; Meneja Mwandamizi wa masuala ya Ubia, Manace Ndoroma; Meneja Mwandamizi wa Usalama, Suleiman Machira na wafanyakazi wengine kutoka katika menejimenti ya GGML, wakimsikiliza Katibu Mkuu wa Wizara ya Madini, Adolph Nduguru.

Katibu Mkuu Wizara ya Madini, Adolph Nduguru akiwa katika picha ya pamoja na Menejimenti ya GGML.
**

Na Mwandishi wetu

KATIBU Mkuu wa Wizara ya Madini, Adolph Ndunguru ameipongeza Kampuni ya (GGML) kwa kuzingatia sheria zinazosimamia sekta ya madini na kutekeleza majukumu yake kwa uweledi.

Ndunguru ametoa kauli hiyo majuzi wakati akizungumza na Menejimenti ya GGML baada ya kufanya ziara katika kampuni hiyo kwa mara ya kwanza.

“Tangu Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan aliponiteu kwenye wadhifa huu, nimesikia maoni mengi mazuri kuhusu GGML.

“Nakumbuka hivi karibuni mlipokea zawadi na tuzo nyingi kule mkoani Dar es Salaam. Tuzo hizo zilikuwa zinatambua utendaji kazi wenu kama kampuni bora ya uchimbaji madini kwa mwaka 2021.

“Ndio maana nimeona ni vyema kutembelea mgodi huu ili kuona kazi nzuri mnayoifanya,” alisema Ndunguru.

Aidha, Makamu wa Rais wa AngloGold Ashanti anayesimamia miradi endelevu kwa upande wa Ghana na Tanzania, Simon Shayo alimshukuru Ndunguru kwa kutembelea mgodi huo.

Alieleza kuwa GGML itaendelea kuzalisha katika mazingira uendelevu kwa kulipa kodi na kuchangia programu mbalimbali za uwekezaji ndani ya jamii zinazosaidia wananchi wanaozunguka mgodi.

“Tumekuwa na changamoto nyingi katika shughuli zetu ikiwa ni pamoja na kupungua kwa madini yanayochimbwa kupitia uchimbaji wa wazi katika mgodi wa Nyankanga.

“Pia kulikuwa na ucheleweshaji wa utoaji wa vibali vya uchimbaji wa wazi Mlima wa Geita na Nyamulilima.

Tunashukuru kwamba sasa tuko katika hatua nzuri kwani uendelezaji wa miradi yote miwili ulianza mwaka 2021.

GGML pia imepata leseni na kuanza kazi ya utafiti madini katika maeneo ya vijijini yaliyopo katika mikoa ya Singida, Dodoma, Kishapu na Nzega,” alisema Shayo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments