MAFUNZO YA UVIKO 19 KWA WADAU WA SEKTA YA UTALII YAZINDULIWA MBEYA


Kaimu Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya Dkt. Salum Manyatta (aliyesimama) akizungumza alipokuwa akifungua rasmi mafunzo hayo katika ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Jijini Mbeya. (kushoto) ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Taifa Dkt. Shogo Mlozi Sedoyeka, na (kulia), ni David Mulabwa, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Mkoa wa Mbeya.
Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya na Kaimu RAS wa Mkoa huo Dkt. Salum Manyatta alipokuwa kwenye mahojiano maalum na Waandishi wa habari
Dkt. Shogo Mlozi Sedoyeka (aliyesimama) akizungumza wakati wa hotuba yake ya utangulizi wakati ufunguzi wa mafunzo kwa wadau wa Sekta ya Utalii Jijini Mbeya. (wa kwanza kushoto), ni Dkt. Naiman Mbise Mratibu wa Mradi, (wa pili kulia), ni Dkt. Salum Manyatta Naibu Katibu Tawala Mkoa wa Mbeya na (wa kwanza kulia), ni David Mulabwa, Kaimu Katibu Tawala Msaidizi Uchumi na Uzalishaji Mkoa wa Mbeya.
Dkt. Shogo Mlozi Sedoyeka (aliyesimama) akizungumza wakati alipokuwa kwenye mahojiano maalum na Waandishi wa habari (hawamo pichani), mara baada ya kumalizika kwa hafla fupi ya ufunguzi wa mafunzo hayo.
Mratibu wa Mafunzo Dkt. Naiman Mbise akizungumza alipokuwa akitoa salamu za utangulizi katika hafla hiyo. Picha na Hughes Dugilo


Na: Hughes Dugilo, MBEYA.
Chuo Cha Taifa cha Utalii (NCT) kimezindua rasmi mafunzo kuhusu Mwongozo wa kukabiliana na janga la UVIKO 19 kwa wadau walioko katika mnyororo wa sekta ya utalii na ukarimu katika mkoa wa Mbeya na Iringa.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Mafunzo hayo Mkoani Mbeya  Afisa Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Utalii, Dk. Shogo Mlozi Sedoyeka amesema kuwa mafunzo hayo yanalenga kusaidia Sekta ya Utalii kwa kuhakikisha kila mdau anapata uelewa sahihi wa namna ya kukabiliana na janga hilo.

"Janga la UVIKO 19 limeathiri kwa namna moja au nyingine Sekta ya Utalii ndiyo maana Cho cha Taifa cha Utalii chini ya Wizara ya Maliasili na Utalii, tunatoa mafunzo haya ili kuwajengea uwezo wadau waliopo katika mnyororo wa Sekta hii kupata uelewa sahihi wa namna ya kukabiliana na janga hili" ,amesema Dkt. Sedoyeka.


Aidha Dkt. Sedoyeka amesema kuwa mafunzo hayo yamekuja kutokana na jitihada kubwa za Rais Samia Suluhu Hassan katika kukabiliana na janga la UVIKO 19 kwa kufadhili mafunzo hayo kupitia mpango wa maendeleo kwa ustawi wa Taifa na Mapambano dhidi ya UVIKO 19.

“Rais Samia suluhu Hassan mbali na kuzipatia fedha Sekta mbalimbali ikiwamo ya Elimu, Afya, Maji na Miundombinu, lakini pia hakuisahau Sekta hii ya Utalii ambapo kupitia fedha za Uviko 19 tumenufaika pia”, ameongeza Dk. Sedoyeka.

Ameeleza kuwa Mafunzo hayo yanatolewa katika mikoa nane ya Tanzania bara ambayo ni Mbeya, Iringa, Ruvuma, Mara,Lindi, Mtwara, Njombe na Mwanza ambapo mpaka sasa tayari mafunzo hayo yameshatolewa katika mikoa ya Lindi na Ruvuma na kwamba kwa sasa mafunzo hayo yanaendelea katika mikoa ya Iringa na Mbeya.

Akifungua mafunzo hayo, kwa niaba ya Katibu Tawala wa Mkoa wa Mbeya, Dk. Angelina Lutambi, Mganga Mkuu wa Mkoa, Dk. Salum Manyatta amesema kuwa ugonjwa wa UVIKO 19 ulichangia kwa kiasi kikubwa kupunguza idadi ya watalii nchini ambapo mwaka 2019 Tanzania ilipokea watalii milioni 1.5 na kwamba baada ya kuripotiwa janga la Corona mwaka 2020 idadi ilishuka hadi kufikia watalii 602,800.

Aliongeza kuwa licha ya kikwazo cha ugonjwa huo, Serikali imeendelea na jitihada mbalimbali katika kukuza utalii kwa kuhakikisha watoa huduma wanapata chanjo pamoja na kuweka miundombinu rafiki ya kukabiliana na ugonjwa huo.

Mafunzo hayo yanafanyika kwa siku tano Mkoani Mbeya na kuudhuriwa na wadau wapatao 150 kutoka katika wilaya zote za Mkoa huo ambapo jumla ya mada sita zitatolewa na wakufunzi mahili na wabobezi kutoka Chuo cha Taifa cha Utalii na kwamba mafunzo hayo yatafikia tamati ijumaa Machi 4, 2022.


PICHA MBALIMBALI ZA MATUKIO WAKATI WA MAFUNZO HAYO

Mganga Mkuu wa Mkoa wa Mbeya na Kaimu RAS wa Mkoa huo Dkt. Salum Manyatta (kulia) akiteta jambo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Utalii Dkt. Shogo Mlozi Sedoyeka (kushoto) wakati wa hafla fupi ya kufungua rasmi mafunzo hayo Mkoani Mbeya.

Afisa Mtendaji Mkuu wa Chuo cha Taifa cha Utalii Dkt Shogo Mlozi Sedoyeka (kulia) akizungumza na Mratibu wa Mradi wa mafunzo hayo Dkt. Naiman Mbise (kushoto) wakati wa hafla fupi ya kufungua rasmi mafunzo hayo yanaendelea katika ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Jijini Mbeya.

Mkufunzi Mwandamizi, na mtaalamu wa Lugha kutoka Chuo cha Taifa cha Utalii Mwl. Pepetua Ishika akifundisha mbinu za Mawasiliano katika kipindi hiki cha UVIKO 19 kwa wadau na washiriki wa mafunzo hayo Jijini Mbeya.



Wadau na washiriki walioudhuria mafunzo hayo wakifuatilia mada mbalimbali zilikuwa zikitolewa na wakufunzi wakati wa mafunzo hayo katika ukumbi wa Chuo cha Uhasibu Mbeya.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments