HISTORIA YA MAADHIMISHO YA SIKU YA REDIO DUNIANI FEBRUARI 13

Historia ya Maadhimisho ya siku ya Redio Duniani Februari 13 

Ikiwa kesho Februari 13 Dunia itaadhmisha SIKU YA REDIO DUNIANI nimepata muda kidogo kuandika historia juu ya maadhimisho ya siku hii. Lengo kubwa ni kutunza historia ya siku hii, takribani ikiwa imepita miaka 11 tangia siku hii ianze kuadhimishwa.

Ifuatayo ni historia ya siku hii katika sura ya ki dunia

Shirika la Elimu, Sayansi na Utamaduni la Umoja wa Mataifa UNESCO lilianzisha Siku ya Redio Duniani kunako mwaka 2012 mara baada ya Baraza Kuu la Unesco kutambua umuhimu wake na mwaka uliofuata Umoja wa Mataifa ukatambua kama Siku ya Redio duniani. Hata hivyo kwa kuthibitisha kuwa, kila tarehe 13 Februari itakuwa inaadhimishwa kutokana na kwamba, tarehe hiyo mwaka 1946 ndipo ilianzishwa Radio ya Umoja wa Mataifa. Ni katika kutumia chombo hiki cha mawasiliano na msingi wa kutoa habari ambayo inasaidia kukuza uhuru wa kujieleza na usawa wa kila kitu. Radio iweze kutoa mchango katika mijadala ya kidemokrasia kwa njia ya kubadilishana mawazo kati ya watangazaji na wasikilizaji. Kwa maana hiyo Redio imekuwa ni nguzo kuu ya kijamii inayoendelea na iliyo endelea duniani kote.


 Kwa nini redio ni muhimu? 

 Velentzas (2014) anaielezea redio kuwa, ni chombo cha kuzalisha mawazo mapya na fikra pevu kwenye kupanua mitazamo ya pamoja kupitia jamii inayobadilishana jumbe mbalimbali ambazo zinajikita kwenye kubadilisha taarifa na mawazo mapya.


 Ni ipi nguvu ya redio?

1.Redio inawafikia watu wengi kwa mara moja kuliko chombo kingine cha habari.

2.Redio inaifikia jamii tofauti ikiwe ni ile yenye utajiri na ile yenye umaskini bila ubaguzi wowote.

3.Redio inaelimisha na kufunza kwenye jamii mbalimbali juu ya mambo muhimu.

4.redio inaaminika zaidi kuliko chombo kingine cha habari na ndio maana ina wasikilizaji wengi.


 Faida kubwa ya redio

Faida kubwa unaweza kusikiliza redio sehemu yoyote ukiwa unafanya jambo lolote lile  kama, wakati ukiendesha gari, ukitembea na hata wakati unapika .


 Wajibu wa redio

Redio inasimama na kuwa moyo wa mawasiliano ndani ya jamii, kwa kuunganisha nguzo kuu tatu ndani ya Taifa yani state Actors ikiwa ni serikali, sekta binafasi na AZAKI.

Redio inawasilisha maudhui mbalimbali kupitia vipindi vyake na kubeba ajenda za maendeleo.

Redio inaboresha mazingira ya kijamii kwenye mfumo wa jamii husika.

Redio inatengeneza jukwaa la pamoja kwenye kusikiliza na kutatua kero mbalimbali kwa kuleta maafisa wa serikali, waathirika wa huduma mbalimbali na watoa huduma zinazokosekana.

Redio zinatemgeneza jukwaa la uchechemuzi wa masuala mbalimbali ya kisera na sheria.

Redio inatengeneza jukwaa la maoni kwa wananchi juu ya watawala na wataliwa kwenye nyakati za uchaguzi.

Redio ni chombo cha sauti ya wasio na sauti, hasa toka maeneo ya vijijini  ambapo redio utumika kupaza sauti za watu wasio na sauti ndani ya jamii na waliobezwa.

Redio inakuza lugha ya kiswahili mfano ni kipindi cha Lulu za Kiswahli kinachorushwa na redio TBC 

Redio inawajibu wa kutumika kama chombo cha kutoa elimu kwenye majanga mbalimbali ikiwemo UVIKO 19 na majanga mengine.

kwa ufupi mimi bado naamini kuwa, redio itabaki kuwa chombo cha habari chenye ngivu sana Duniani.

Nawatakia maadhimisho mema watangazaji wote wa redio. Kikubwa ni kukumbuka kuwa mna jukumu kubwa na mnapaswa kutumia vyema vipasa sauti vyenu na kulinda maadili ya utangazaji.

 Edwin Soko - Media specialist

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments