JESHI LAPINDUA SERIKALI...RAIS WA BURKINA FASO HAJULIKANI ALIPO


Jeshi limesema hali mbaya ya usalama ndio iliolishinikiza kumuondoa madarakani rais Kabore


Jeshi nchini Burkina Fasso linasema kwamba limechukua mamlaka na kumuondoa madarakani rais Roch Kabore.

Tangazo hilo lilitolewa katika runinga ya taifa na afisa mmoja wa jeshi , ambaye alisema kwamba serikali na bunge limevunjwa.

Kufikia sasa haijulikani bwana Kabore yuko wapi , lakini afisa huyo amesema kwamba wale wote wanaozuiliwa wapo katika eneo salama.

Mapinduzi hayo yanajiri siku moja tu baada ya wanajeshi hao kudhibiti kambi za jeshi huku milio ya risasi ikisika katika mji mkuu wa Ouagadougou..

Mapema , Chama tawala cha peoples Movement PMP kilisema kwamba wote Kabore na waziri mmoja wa serikali walinusurika jaribio la mauaji.

Siku ya Jumapili, wanajeshi waasi walitaka kufutwa kazi kwa maafisa wa jeshi na kuongezwa kwa raslimali za kukabiliana na wapiganaji wa Kiislamu.

Taarifa hiyo ilitolewa na kundi ambalo halijasikika hapo awali, Vuguvugu la Patriotic for Safeguard and Restoration au MPSR, kifupi chake cha Kifaransa.

"MPSR, ambayo inajumuisha vitengo vyote vya jeshi, imeamua kusitisha wadhifa wa Rais Kabore leo," ilisema.

Kabla ya tangazo hilo, Muungano wa Afrika na Umoja wa Afrika Magharibi Ecowas walilaani kile walichokiita jaribio la mapinduzi nchini Burkina Faso.


Ecowas imesema kwamba wanajeshi watawajibikia usalama usalama wa Bw Kaboré iwapo lolote litatokea.
Rais Roch Kabore

Video kutoka mji mkuu inaonekana kuonyesha magari ya kivita - yanayoripotiwa kutumiwa na rais - yakiwa na mashimo ya risasi na kutelekezwa mitaani.

Huduma za mtandao wa simu za mkononi zimekatizwa, ingawa mtandao wa laini zisizobadilika na wi-fi ya nyumbani zinafanya kazi

Bw Kaboré hajaonekana hadharani tangu mzozo huo uanze lakini machapisho mawili yalionekana kwenye akaunti yake ya Twitter kabla ya afisa huyo kutangaza kuwa amepinduliwa.

Baadaye alitoa wito kwa wale waliochukua silaha kuziweka chini "kwa maslahi ya taifa". Hapo awali Bw Kaboré alipongeza timu ya taifa ya kandanda kwa ushindi wao katika mechi ya Kombe la Mataifa ya Afrika.

Haijulikani ikiwa Bw Kaboré au mtu mwingine alichapisha tweets hizo.

Baadhi ya vyanzo vya usalama vinasema rais na mawaziri wengine wa serikali wanazuiliwa katika kambi ya Sangoulé Lamizana katika mji mkuu.

Siku ya Jumapili, mamia ya watu walijitokeza kuwaunga mkono wanajeshi hao na baadhi yao walichoma moto makao makuu ya chama tawala. Amri ya kutotoka nje wakati wa usiku imewekwa.

CHANZO - BBC SWAHILI

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments