AJIUA KWA KUJICHOMA MOTO MBEYA


JESHI LA POLISI MKOA WA MBEYA LINAWASHIKILIA WATUHUMIWA 114 KWA TUHUMA ZA MAKOSA MBALIMBALI YAKIWEMO YA KUPATIKANA NA DAWA ZA KULEVYA, POMBE HARAMU YA MOSHI, WAHAMIAJI HARAMU NA MAKOSA YA KUJIHUSISHA NA UHALIFU WA AINA MBALIMBALI.

AJIUA KWA KUJICHOMA MOTO.

Mnamo tarehe 08.11.2021 majira ya saa 03:00 asubuhi huko Kijiji cha Ihombe kilichopo Kata ya Utengule Usongwe, Tarafa ya Usongwe, Wilaya ya Mbeya Vijijini, Mtu mmoja aliyefahamika kwa jina la MASHAKA SAIMON @ YOKONIA [35] Mkazi wa Kijiji cha Ihombe alikutwa ndani ya nyumba yake akiwa amefariki dunia kwa kuungua moto.

Ni kwamba kabla ya tukio hilo marehemu alikuwa akisumbuliwa na maradhi kwa muda mrefu na alitelekezwa na mke wake hali iliyopelekea kukata tamaa ya maisha na siku chache zilizopita alifanya jaribio la kujilipua kwa Petrol kabla ya kuokolewa na mdogo wake. Upelelezi wa shauri hili unaendelea.

Aidha ninatoa wito kwa wananchi/jamii kwa ujumla kutoa taarifa za mtu/watu wenye hali ya kukata tamaa ya Maisha kwa viongozi wao wa vijiji, mitaa kabla ya kutokea madhara makubwa kama ilivyotokea kwa marehemu MASHAKA SAIMON @ YOKONIA.


KUPATIKANA NA MADAWA YA KULEVYA.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia watuhumiwa wawili 1. RAMADHAN ABAS ISSA [45] mkazi wa kyela kati na 2. FRANK MGAYA [22], mkazi wa mikumi – Kyela wakiwa na kete mbili za unga unaodhaniwa kuwa ni dawa za kulevya aina ya heroine wenye uzito wa gram 1.

Watuhumiwa walikamatwa mnamo tarehe 08.11.2021 majira ya saa 02:45 usiku huko maeneo ya Kyela kati, Kata ya Kyela, Tarafa ya Unyakyusa, Wilaya ya Kyela, Mkoa wa Mbeya katika misako inayoendelea maeneo mbalimbali ya mkoa wa mbeya dhidi ya wauzaji, watumiaji na wasambazaji wa dawa za kulevya.

KUINGIA NCHINI BILA KIBALI.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limefanikiwa kuwakamata wahamiaji haramu watano wote raia wa nchini Rwanda kwa kosa la kuingia nchini bila kibali. Watuhumiwa waliokamatwa ni:- 1. FENIAS ENOCK [26] 2. PONTIEN SHYRAKERA [23] 3. MUNIZERO EDITE [13] 4. LASUBIZA ISHIVINIELA [11] na 5. LATUS LOUANJA [09].

Watuhumiwa walikamatwa mnamo tarehe 08.11.2021 majira ya saa 03:30 asubuhi huko kwenye kizuizi cha Polisi kilichopo Igurusi, Kata ya Igurusi, Tarafa ya Ilongo, Wilaya ya Mbarali, Mkoa wa Mbeya. Taratibu za kisheria zinaendelea kwa kushirikiana na idara ya uhamiaji.

KUPATIKANA NA POMBE MOSHI @ GONGO.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia RHODA MWASOMOLA [64] mkazi wa Mwasote Jijini Mbeya akiwa na pombe moshi @ gongo lita tano [05]

Mtuhumiwa alikamatwa mnamo tarehe 08.11.2021 majira ya saa 08:30 mchana huko Mtaa wa Mwasote, Kata ya Itezi, Tarafa ya Iyunga, Jijini Mbeya katika misako inayoendelea Jijini hapa. Mtuhumiwa alikutwa akiwa ameficha pombe hiyo haramu kwenye dumu la lita tano na kwenye kichupa kidogo cha valeur.

KUPATIKANA NA BHANGI.
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia watuhumiwa wawili 1. EXPEDITO MAKUNGU [38] mkazi wa mlowo na 2. NGALA MAYOMBO [30] mkazi wa Ifakara – Morogoro wakiwa na dawa za kulevya aina ya bhangi debe mbili na kete 315 sawa na uzito wa kilogram saba [07].

Watuhumiwa walikamatwa mnamo tarehe 08.11.2021 majira ya saa 01:30 usiku huko Kitongoji cha Matanda, Kijiji cha Itumbi, Kata ya Matundasi, Tarafa ya Kiwanja, Wilaya ya Chunya, Mkoa wa Mbeya. Watuhumiwa ni wauzaji na watumiaji wa dawa hizo za kulevya.

KUFANYA KAZI YA UGANGA WA JADI BILA KIBALI.

Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linamshikilia HUSSEIN MOHAMED [42] mkazi wa Sumbawanga Mkoa wa Rukwa kwa tuhuma za kufanya kazi za uganga wa kienyeji bila kuwa na kibali.

Mtuhumiwa alikamatwa mnamo tarehe 07.11.2021 majira ya saa 12:15 jioni huko maeneo ya Iyunga, Jijini Mbeya akiwa kwenye nyumba ya kulala wageni iitwayo “Liliz” akifanya kazi za uganga wa kienyeji bila kuwa na kibali cha kufanya shughuli hizo.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments