SERIKALI YAWEKA MKAKATI KUENDELEA KUMLINDA MKULIMA, YATOA MILIONI 700 UJENZI SKIMU YA USENSE MKOANI KATAVI


Naibu Waziri wa Kilimo akizungumza na wakulima wa skimu ya umwagiliaji ya Usense Halmashauri ya wilaya ya Nsimbo mkoani Katavi jana wakati alipokagua skimu hiyo ambayo serikali imetoa kiasi cha shilingi milioni700 kwa ajiliya kuijenga upya.

Naibu Waziri wa Kilimo akielekeza jambo wakati alipokagua skimu ya umwagiliaji ya Uense wilayani Nsimbo mkoa wa Katavi jana.

**********

Na Mwandishi Wetu

NAIBU Waziri wa Kilimo Hussein Bashe amesema Serikali ya awamu ya sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan, itamlinda mkulima kwa kuhakikisha kilimo kinabadilisha yao, huku akielezea hatua ambazo zinachukuliwa kuboresha Skimu ya Umwagiliaji Usense iliyopo wilayani Mpanda mkoani Katavi.

Bashe ametoa kauli hiyo wakati alipotembelea na kukagua Skimu ya umwagiliaji ya Usense na Msaginya katika Kata ya Uruwira Wilaya ya Mpanda mkoani Katavi. Akifafanua zaidi mbele ya wakulima wanaofaidika na Skimu hiyo amesema, wameweka mkakati ambao utamlinda mkulima,lengo ikiwa ni kuhakikisha wakulima wananufaika kupitia shughuli zao za kilimo.

Naibu Waziri huyo amesema pia, Rais Samia ametoa Sh.Milioni 700, ili kujengwa kwa skimu hiyo ya Usense na kuboresha uzalishaji wa zao la mpunga linalolimwa katika skimu hiyo.

"Ni dhambi kuwaletea matumaini ambayo hayapo utaratibu uko hivi nimempa Mhandisi siku 45 na zabuni iwe imetangazwa ,watafanya michakato yao kumpata mkandarasi kwa hiyo hii skimu hii yenye wakulima 250 haitaanza kujengwa leo itachukua muda hadi kukamolika ujenzi wake.

“Ninaamini msimu huu hata ukianza skimu haitakuwa imejengwa kwa sababu miujiza ilikuwepo wakati wa mtume Muhammad na Yesu, siku hizi hakuna miujiza,"amesema Bashe na kusisitiza lazima taratibu ziwepo kufanikisha ujenzi.

Ameongeza kuwa, skimu hiyo itajengwa mfereji mkuu ambao utakuwa na kilomita 8 na mifereji mitano ambayo itakuwa na kilimota 7.5 kwa hiyo wakulima hao wasubiri, hata hivyo amewahakikishia zabuni itatangazwa ndani ya siku 45 na mkandarasi lazima apatikane.

"Nataka kupata majibu katika kipindi kifupi kwamba mkandarasi tayari amepatikana na taratibu zote zinaendelea vizuri, tunataka kila kitu kiwe sawa ili Waziri aje kuzindua ujenzi wa skimu hii.Serikali itawekeza fedha hizo milioni 700 ili kujenga hii skimu ya Usense."amesema.

Pia ametoa maagizo kwa Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Nsimbo mkoani Katavi kuhakikisha wakulima waliosajiriwa kwenye skimu hiyo wanapimiwa maeneo yao na kupewa hati ya umiliki wa mashamba, kila mtu awe na hati ya umiliki wa shamba lake ili wawe na uhakika ili wawe na uchungu wa kutunza maeneo yao.

Bashe amesema Serikali imeanzisha Mfuko wa Kuendeleza Umwagiliaji, hivyo wakulima wa kilimo cha umwagiliaji watapewa elimu kuhusu mfuko ambapo wakivuna mazao kuna mchango ambao watautoa kuchangia, na fedha hizo zinawekwa kwenye mfuko kwa ajili ya kusaidia kufanyika matengenezo ya banio pale litakapoharibika.

"Mkulima asilazimishwe kulipa fedha kama hajalipa kiingilio cha kujisajili, mnaweza mkakubaliana mkulima akivuna kama ni asilimia 2.5 au 3 mpige mahesabu kwa gunia za mpunga halafu zile gunia zinahifadhiwa kwenye ghala la pamoja,"amefafanua Bashe.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments