SERIKALI KUANGALIA MFUMO WA UTAWALA WA SHERIA KUONDOA VIKWAZO VYA UWEKEZAJI



Na Dotto Kwilasa, DODOMA.

SERIKALI imesema itakaa na kuangalia upya mfumo wa utawala wa Sheria katika ngazi za Halmashauri ili kuondoa vikwazo na migongano kwa wawekezaji hali itakayo chochea na kuongeza uwekezaji nchini.


Hatua hii imekuja kufuatia vijana wawekezaji wa masuala ya kilimo kupitia kampuni ya umma ya "Jenga Afya Tokomeza Umasikini (JATU PLC)"
kuitupia lawama Mifumo ya sheria na utawala katika serikali za mitaa kuwa ni moja ya changamoto kubwa inayokwamisha juhudi za uwekezaji huku wakiomba Serikali kuingilia kati suala hilo.

Akiongea usiku wa kuamkia leo Oktoba 24,2021 Jijini Dodoma katika maadhimisho ya miaka mitano ya kampuni ya umma ya Jenga Afya Tokomeza Umaskini (JATU PLC) ambayo inayowaunganisha wakulima na kuwawezesha kujihughulisha na uwezeshwaji wa vijana masuala ya kilimoWaziri wa Sera,Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na walemavu,Jenister Mhagama alisema Serikali haiwezi kukubali mfumo wa kiutawala uliopo kwani unakwamisha juhudi za kuwakwamua watanzania.

"Natoa rai kwa viongozi wa Serikali wote kutoka ngazi ya Taifa mpaka ya kijiji kuhakikisha mifumo tuliyonayo ya kiutawala isiwe kikwazo cha maendeleo kwasababu ya maelekezo tofauti tofauti ya viongozi ,Serikali haiwezi kukubali mfumo huu ,tunataka watanzania waondokane na umasikini ;

"Utakuta Dc anasema kingine,Mkurugenzi anasema kingine,mwenyekiti wa kijiji anasema kingine na mwenyekiti wa kata na mtaa anasema kingine haiwezekani kwasababu tutakuwa tumepoteza nguvu kazi hii ambayo inaingia kazini kuleta matokeo chanya na kuleta mabadiliko ndani Taifa,"amesema.

Aidha Mhagama ameeleza kuwa mara ya kwanza kukutana na vijana wa Jatu alikuwa anajiuliza kwa wiki nzima kama wataweza walichokianzisha lakini kutokana na mkutano huo wa maadhimisho wamemthibitishia kuwa wametimiza miaka mitano yenye mafanikio kwasababu walikuwa na dhamira njema kwa Taifa nzima.

"Leo nilipokuwa nakuja nilikuwa nategemea kusikia vitu ambavyo nimezoea kuvisikia ninapokutana na Jatu na vijina jambo kubwa ambalo walikuwa wakinipa ni changamoto hii mara tumeshindwa kupata hiki,hatujawezeshwa hiki,hatujasaidiwa hiki,hatujaonyeshwa hiki lakini mkutano huu umekuwa wa tofauti umetukutanisha kutueleza fursa,"amesema.

Amesema pamoja na changamoto ambazo tayari wameshazifanyiakazi na ambazo zimebaki ni zakwake yeye ambazo ametakiwa andoke nazo ili kwenda kuzifanyia kazi.

"Baada ya kutoka hapa lazima nikaangalie Sera zangu nijue zinasema nini ili niweze kuwawezesha vijana,pia nikaangalie sheria zinazowagusa vijana pamoja na kuangalia programu zote zilizo ndani ya serikali zilizowekwa je zinamazingira mazuri yakuwafanya vijana kuweza kutengeneneza nia na kiu yao yakulifanya Taifa hili liondokane na umasikini lakini kwa mipango na kweli hizi ambazo tupo nazo ndani ya nchi,"ameeleza.

Pamoja na hayo ametoa maagizo kwa viongozi wa Ofisi ya waziri mkuu,watu wa soko la hisa,kwamba ndani ya wiki moja wahakikishe wanakaa wanatengeneza mkakati
fungamanishi.

Amesema ndani ya serikali wanayo mikakati ya tayari ambao alitaja kilimo na viwanda lakini alisema wanahitaji watu watakao tengeneza mikakati hiyo ya serikali kwa kuitafsiri kwa vitendo na dhamira kama ambavyo tayari Jatu wamefanya hivyo.

Kwa upande wake Katibu Mkuu wa JATU PLC Issa Simbano amesema kampuni ya JATU imefanikiwa kuajiri vijana wa kike na kiume wenye umri chini ya miaka 35 wapatao 500 ikiwa ni ajira za moja kwa moja (direct employment), na zaidi ya ajira 10,650 (indirect employment) zimetengenezwa na kuwanufaisha
wazee, akina mama na vijana wa kitanzania kupitia shughuli za kila siku zinazofanyika katika maeneo iliyopo miradi ya kampuni.

Ameongeza kuwa kodi ya serikali; kampuni imefanikiwa kuingia katika mifumo bora ya utawala wa kisheria na inaendeshwa kwa kuzingatia sheria zote za nchi ikiwa ni pamoja na kuhakikisha inasimamia vyema ukusanyaji na ulipaji wa kodi ya serikali.

Licha ya hayo amesema kwa kipindi cha miaka mitano wamekuwa na baadhi ya changamoto ambazo kwa namna moja ama nyingine zimerudisha nyumba spidi ya ukuaji wao huku akizitaja baadhi ya changamoto hizo ni pamoja na ukosefu wa uelewa wa kutosha katika jamii kuhusu elimu ya biashara, sheria na dira
ya kampuni hiyo.

"Kampuni ya JATU inafanya miradi shirikishi ambayo inashirikisha
watu kutoka jamii mbalimbali na bila kujali ukubwa wa uelewa wa watu hao au ngazi ya kipato chao,hali hii inapelekea kampuni kuwa na watu tofauti tofauti,
kupitia mchanganyiko huu tumejikuta tunao watu baadhi ambao hawana uelewa wa
kutosha kuhusu uchumi shirikishi kama vile elimu ya hisa, bima na kilimo cha pamoja,"ameeleza.

Amesema hali hiyo inachangia changamoto katika kampuni hasa inapofika wakati ambao kuna jambo ambalo linahitaji kutatuliwa kwa utashi wa ufahamu wa mfumo wa biashara wanaotumia.

"Watu wa namna hii huwa wanaishi kwa wasiwasi sana kwani bado wanapata ugumu kuamini kama mifumo hii ni salama,kutokana na hali hii watendaji tumekuwa tukitumia muda mwingi kutoa elimu na miongozo ili kupata
uelewa wa pamoja,tunaamini kama jamii yetu ingekuwa na uelewa wa kutosha, basi
tungetumia muda mwingi kufikiria namna ya kuibua fursa na miradi mingi zaidi,"amesisitiza.

Mbali na hayo Katibu huyo ameitupia lawama Mifumo ya sheria na utawala katika serikali za mitaa kuwa ni moja ya changamoto kubwa iliyopo katika taifa hasa ngazi ya serikali za mitaa na kueleza kuwa sheria na
utawala bora bado ni janga lililopo kwa viongozi wengi wa serikali katika ngazi za halmashauri na wilaya .


Naye Mkurugenzi Mtendaji wa JATU PLC Peter Isore ameeleza kuwa ili kuinua sekta ya Kilimo Kampuni hiyo imekuwa ikiwajengea uwezo na ufahamu vijana waanzilishi wa JATU baada
ya kushiriki shindano la mwaka 2016 na kuwapa malezi mema na miongozo bora ambayo imewezesha kampuni kukidhi matakwa ya sheria na kanuni za kuuza hisa kwa umma, kuongeza mtaji na hatimaye kuorodheshwa katika soko la hisa la Dar es salaam.

Ameongeza kuwa malengo ya kampuni hiyo
yanaendana sambamba na malengo makuu ya serikali ya kuhakikisha inaboresha maisha ya kila mtanzaniana kwamba watahakikisha wanatimiza malengo kwa kuimarisha lishe na usalama wa chakula katika jamii yetu,kuanzisha miradi mingi ya kisasa na shirikishi ya kilimo na ufugaji katika maeneo yenye ardhi stahiki na kuanzisha viwanda karibu na mashamba ya wakulima ili kupunguza gharama za
kusafirisha malighafi kwa wakulima kutoka shambani kwenda sokoni.

"Tumelenga pia kuibua na kuimarisha masoko kwa kutumia TEHAMA, kutengeneza kipato na ajira ya kudumu kwa kila mtumiaji wa bidhaa za chakula
kupitia mfumo wa masoko ya mtandao ambao unatoa gawio la faida kwa wateja kila mwezi, kuwezesha upatikanaji wa mitaji na bima katika kutekeleza miradi ya kiuchumi ili kutokomeza umaskini na kuibua na kulea mawazo ya vijana wabunifu ili yaweze kuzalisha huduma na ajira
nyingi zaidi katika jamii,"amefafanua.

Amesema Kampuni hiyo imekuwa ikiwakutanisha watu wenye mitaji na fursa mbalimbali za kiuchumi na kuwapa elimu
ya namna ya kuwekeza na kunufaika kwa pamoja katika kilimo, viwanda na Tehama (masoko) na kupata mafanikio .


Ametaja baadhi ya mafanikio hayo kuwa ni kilimo jumuishi ambacho kinajumuisha wanahisa wake ambao kwa ushirikiano, kampuni inatafuta maeneo mazuri ya uwekezaji na kwa makubaliano mazao pendekezwa hulimwa kwa kutumia teknolojia na wataalamu sahihi wa kilimo ili kupata mavuno bora ambayo huuzwa katika viwanda vya kampuni kama malighafi.


"Kwa kipindi cha miaka mitano 2016-2021; kampuni imewawezesha wanachama wake wapatao elfu tano (5000) kulima zaidi ya ekari 47,000 za mazao ambayo ni mahindi, mpunga, alizeti, maharage, machungwa na parachichi kwa mikoa ya Tanga, Morogoro, Njombe na Manyara, Wakulima wote wanalima kwa mikopo nafuu inayotolewa bila riba kupitia JATU Saccos Ltd (JSL), ambayo ni saccos iliyoanzishwa nasi ili kuwarahisishia wakulima gharama za kilimo,"anaeleza.


Pamoja na mambo mengine amesema,hadi kufikia sasa kampuni imefanikiwa kumiliki mashine za kisasa katika kilimo kama vile matrekta ya kulima na mashine za kuvunia na tayari tumeanza kutengeneza miundombinu ya umwagiliaji katika baadhi ya mashamba ili kukifanya kilimo chenye tija muda wote bila kuathiriwa na majira au mabadiliko ya tabia nchi.


"Kwa upande wa Viwanda,kampuni imeanzisha viwanda vya kati ambavyo vinachakata mazao yote yanayolimwa na wanachama wake, mfano wa viwanda hivi ni pamoja na kiwanda cha kuchakata mchele kilichopo Kilombero Morogoro na kiwanda cha unga wa mahindi dona na sembe pamoja na mafuta ya alizeti kilichopo Kibaigwa Dodoma, pia kampuni ina vituo vingine vilivyopo maeneo ya miji kwa ajili ya kusafisha na kufungasha bidhaa mbali mbali ambazo zinauzwa na kampuni kama vile maharage na karanga,"amesema.

Vilevile Mkurugenzi huyo amesema kwa upande wa Masoko, kampuni ya JATU inatumia TEHAMA kuendesha mfumo mkubwa wa
masoko, mfumo ambao unatengeneza ajira nyingi kwa vijana kwa mfumo wa kuwalipa commission kulingana na wanavyouza bidhaa.
Baadhi ya wawekezaji wa masuala ya Kilimo wakisikiliza kwa makini fursa zinazotolewa na Kampuni ya JATU PLC 
katika maadhimisho ya miaka mitano ya kampuni hiyo yaliyofanyika Jijini hapa kwa lengo la kuchochea juhudi za Serikali katika kuinua Uchumi wa viwanda.
Waziri wa Sera,Bunge,Kazi,Vijana,Ajira na walemavu Jenister Mhagama akiongea 
katika maadhimisho ya miaka mitano ya kampuni ya umma ya Jenga Afya Tokomeza Umasikini (JATU PLC)ambayo inayowaunganiaha wakulima vijana .

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments