RAIS SAMIA KUZINDUA MKAKATI WA UELIMISHAJI, UHAMASISHAJI MASUALA YA SENSA

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka 

Na Dotto Kwilasa, Dodoma
SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Ofisi ya Taifa ya Takwimu inatarajia kuzindua Kitabu cha Mkakati wa uelimishaji na uhamasishaji wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022 jijini Dodoma huku Rais Samia Suluhu Hassan akitarajiwa kuwa mgeni rasmi kwenye uzinduzi huo.

Mkuu wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka amethibitisha hayo leo wakati akiongea na waandishi wa habari kuhusu ujio wa tukio hilo ambapo alisema linalenga kuandaa umma na wadau kwa ujumla kwa ujio wa sensa ya watu na makazi ya mwaka ujao.

Mtaka amesema pamoja na Rais Samia,uzinduzi huo pia utahudhuriwa na Viongozi mbalimbali akiwemo Waziri Mkuu Kassim Majaliwa,Mwenyekiti wa kamati ya Kuu ya sensa Tanzania bara na visiwani na Makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar Hemed Suleiman Abdallah.

Viongozi wengine ni "Kamisaa wa sensa Tanzania Bara ,Anne Makinda,Kamisaa wa sensa Zanzibar ,Balozi Mohamed Haji Hamza ,pamoja na Mawaziri,Manaibu Waziri ,Makatibu wakuu ,Manaibu katibu wakuu na viongozi wa serikali kutoka Mikoa minne,"amesema na kuongeza;

"Viongozi wa serikali kutoka Mikoa minne watashiriki,Mkoa wa Singida,Iringa, Morogoro na Manyara hivyo hata wananchi wa wadodoma wanatakiwa kujitokeza kwa wingi kumuunga mkono Rais wetu kwasababu sensa ni jambo letu wote,"amesema.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Takwimu za Uchumi,Ofisi ya Taifa ya Takwimu ,Daniel Masolwa amesema kutokana jukumu iliyopewa ofisi hiyo,itawajibika kwa ukaribu kuratibu masuala ya sensa kwa kuhusisha madodoso manne.

"Tumeandaa dodoso kuu,dodoso la nyumba,watu pamoja na anuani za makazi, tayari tumeshaandaa sensa ya majaribio ambayo inafanyika katika Mikoa 13,lengo la majaribio hayo ni kupima na kuhakiki vitendea kazi vyetu na ikiwa vitakuwa na changamoto yoyote virekebishwe,"amesema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments