MGEJA AWAPONGEZA MACHIFU KUMSIMIKA RAIS SAMIA 'KUWA CHIFU MKUU WA MACHIFU TANZANIA


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe. Samia Suluhu Hassan, akipokea Mkuki na Ngao kutoka kwa Chifu Fundi Kira Makamu Mwenyekiti wa Umoja wa Machifu Tanzania mara baada ya kusimikwa kuwa Mkuu wa Machifu wote Tanzania na kuitwa jina la Hangaya yani Nyota inayong`aa, katika Tamasha la Utamaduni (Mila na Desturi zetu) lililofanyika Septemba ,08,2021 katika Viwanja vya Redcross Kisesa Magu, Mkoani Mwanza
Khamis Mgeja

Na Baltazar Mashaka - Kahama
MWENYEKITI wa Tanzania Mzalendo Foundation, Khamis Mgeja ameupongeza Umoja wa Machifu Tanzania (UMT) kwa kumpa heshima iliyotukuka Rais Samia Suluhu Hassan baada ya kumsimika kuwa Chifu Mkuu wa Machifu nchini Tanzania.

Alitoa pongezi mjini Kahama, jana alipoombwa na waandishi wa habari kutoa maoni yake kuhusu Rais Samia kusimikwa kuwa Chifu Mkuu wa Watemi nchini na kupewa jina la Hangaya lenye maana ya Nyota Njema.

Mgeja alisema, Machifu kumpa Rais Samia heshima hiyo adhimu iliyotukuka kwenye mila,desturi na utamaduni wa Kiafrika,wanastahili pongezi.

“Nitumie fursa hii pia kumpongeza Rais Samia au Chifu Hangaya kuwa Chifu Mkuu wa Watemi na nina imani atatuongoza vizuri Watanzania ili tuendelee kudumisha na kuenzi utamaduni wetu,mila na desturi,”alisema.

Mgeja ambaye ni mmoja wa wanafamilia ya wanangwa (wasaidizi) wa Chifu Kapela wa eneo la Kijiji cha Nhumbili, Tinde, Wilaya ya Shinyanga , alisema jina alilopewa la Hangaya (Nyota njema/Nyota inayong'aa) ni la heri kubwa kwa Watanzania likiwa na falsafa pana ya heri na mafanikio.

“Majina yote mawili yana heri kubwa ya uongozi katika nchi yetu,ukiunganisha jina la Hangaya na Suluhu, moja linabeba heshima na mafanikio kama nchi na Watanzania wote, la pili la Suluhu linabeba suluhisho la changamoto zinazoikabili nchi na zinazogusa maisha ya Watanzania,”alifafanua zaidi.

Mwanasiasa huyo mkongwe nchini na Mwenyekiti wa zamani wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Shinyanga, pia aliyewahi kuwa Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Taifa (NEC), alisema majina mazuri ya viongozi yana manufaa na heri nyingi, hata viongozi wa dini wamekuwa wakisistiza jamii kuwapa watoto majina mazuri.

Alisema duniani kote nchi zinazoheshimu,kudumisha kuenzi,kurithisisha utamaduni,mila na desturi zao zimepiga hatua kubwa kimaendeleo,kiutamaduni na kimaadili,akatolea mfano China,Japan,Korea,India,Ujerumani na nyingine.

Mwenyekiti huyo wa Mzalendo Tanzania Foundation aliwaomba Watanzania kushirikiana na Serikali ya Awamu ya Sita kwa pamoja kuendeleza na kudumisha utamaduni wetu, ni muhimu sana na lazima lipewe kipaumbele kwa kiwango cha juu na jamii.

Mgeja akimnukuu Hayati Baba wa Taifa, Mwalimu Nyerere, alisema 'Taifa lolote lisilokuwa na utamaduni wake limekufa.

“Hivi sasa Tanzania tulikuwa tukielekea huko na bahati nzuri tumempata Rais msikivu na naamini hatutafika huko na hatutakuwa taifa mfu chini ya Chifu Hangaya,” alisema Mgeja na kuongeza;

“Kama nchi tukitaka kuwa na viongozi wazalendo na waadilifu ni muhimu wakatokana na malezi yanayozingatia mila,desturi na maadili yakiwemo ya dini na wala tusidanganyane, hatuwezi kupata viongozi waadilifu, wazalendo wasipoandaliwa kwenye misingi ya malezi na makuzi yao.”

Aidha kuhusu maombi yaliyotolewa na machifu kwenye hafla ya kumsimika Rais Samia iliyofanyika kwenye Uwanja wa Red Cross Kisesa na kupewa jina la Chifu Hangaya, Mgeja alieleza kuwa, ana imani serikali ya awamu ya sita itafanyia kazi.

Pia alisistiza serikali iendelee kushirikiana kwa karibu na machifu kwani ni watu muhimu na waoaheshimika sana kwenye jamii, wana sauti na ushawishi mkubwa.

Aliongeza kuwa serikali kuwa karibu na machifu ni mwanzo mzuri,hatua hiyo inastahili pongezi na mengine yatafuata ya kudusmisha ushirikiano kwani Tanzania kudumisha ushirikiano na machifu kuwa na utamaduni imara inawezekana,hivyo twende pamoja kulijenga taifa letu.ssss

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments