ULEGA AAGIZA WATENDAJI KUSIMAMIA MAELEKEZO YA VIONGOZI


Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akitoa maelekezo kwa Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko kutoka wizarani Bw. Stephen Michael pamoja na uongozi wa machinjio ya jiji la Dodoma kufanya ukarabati sehemu ya kupakia nyama machinjioni hapo mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ya ukarabati wa machinjio hayo. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).



Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akitoa maelekezo kwa Kaimu Meneja Mkuu wa machinjio ya Jiji la Dodoma Bw. Fabian Maselele (kushoto), wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika machinjio hayo kufuatilia maagizo aliyoyatoa juu ya ukarabati wa machinjio hayo yaliyoanza Tarehe 15 Mwezi Julai mwaka huu ambapo hadi sasa zimetumika Shilingi Milioni 40. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) akikagua baadhi ya vifaa vipya vilivyowekwa katika machinjio ya Jiji la Dodoma, mara baada ya kufanya ziara ya kushtukiza kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ya ukarabati wa machinjio hayo. Kushoto kwake ni Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko kutoka wizarani Bw. Stephen Michael. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akitoa maelekezo kwa uongozi wa machinjio ya Jiji la Dodoma, kukarabati beseni la kuhifadhia damu mara baada ya ng’ombe kuchinjwa wakati alipofanya ziara ya kushtukiza katika machinjio hayo kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ya ukarabati wa machinjio hayo. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).
Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb), akitoa maelekezo kwa uongozi wa machinjio ya Jiji la Dodoma, kukarabati sakafu ya jengo la machinjio hayo wakati alipofanya ziara ya kushtukiza machinjioni hapo kufuatilia utekelezaji wa maagizo aliyoyatoa ya ukarabati wa jengo hilo pamoja na vifaa vya machinjio. (Picha na Edward Kondela, Afisa Habari - Wizara ya Mifugo na Uvuvi).



Na. Edward Kondela

Naibu Waziri wa Mifugo na Uvuvi Mhe. Abdallah Ulega (Mb) amesema atahakikisha kila maelekezo anayoyatoa anayafuatilia kwa karibu ili kujiridhisha na utekelezaji wake na kufikiwa kwa malengo ya serikali.

Naibu Waziri Ulega amebainisha hayo (29.08.2021) wakati alipofanya ziara ya kushtukiza kujionea maendeleo ya ukarabati wa machinjio ya Jiji la Dodoma yaliyoanza Tarehe 15 Mwezi Julai mwaka huu.

Mhe. Ulega amesema ameridhishwa na ukarabati unaondelea kufanywa ambapo hadi sasa zimetumika Shilingi Milioni 40 kwa kutumia mapato ya ndani ya machinjio hayo.

“Kila maelekezo tunayoyatoa, tunayatoa kwa wakati maalum na kinachofuata ni ufuatiliaji wa karibu, tunatoa maelekezo na kufuatilia utekelezaji wake, tunawapongeza watendaji wetu wizarani maana kila maelekezo tunayoyatoa wanayasimamia na mnafanya kazi nzuri maelekezo tunayoyatoa mnayafanyia kazi.” Amesema Mhe. Ulega

Mhe. Ulega amesema alitoa maelekezo ya kuona machinjio ya jiji la Dodoma, yanabadilika na kuwa bora na kwamba ameridhika na ukarabati unaoendelea hadi sasa ambapo awali uongozi wa machinjio ulihitaji Shilingi Bilioni Tatu, lakini aliwaelekeza kuanza kufanya ukarabati kwa kutumia mapato ya ndani.

Amefafanua kuwa yeye kama kiongozi anatoa maelekezo na kuhakikisha yanasimamiwa usiku na mchana na kuyafuatilia hadi mwisho wake na kutaka maboresho hayo yawe yamekamilika kufikia Tarehe 15 Mwezi Septemba mwaka huu.

Kwa upande wake Kaimu Mkurugenzi wa Idara ya Uzalishaji na Masoko kutoka Wizara ya Mifugo na Uvuvi Bw. Stephen Michael amesema hadi sasa ukarabati wa machinjio ya Jiji la Dodoma yamefikia zaidi ya asilimia 90 ambapo maeneo 13 kati ya 15 yatakuwa yamekamilika mwisho wa mwezi huu na maeneo mawili yaliyobakia yatakamilika ifikapo Tarehe 15 Mwezi Septemba

Bw. Michael amesema ni muhimu kwa wao kama watendaji wanaposimamia maelekezo ya viongozi ni kwamba wanajua athari zinazoweza kujitokeza kutokana na ulaji wa nyama isiyo na usalama na kwamba watasimamia ukarabati huo kwa weledi mkubwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments