TSH. TRILIONI 3.6 KUTUMIKA UTEKELEZAJI MIUNDOMBINU YA BARABARA


 Na.Faustine Gimu Galafoni,Dodoma.
Waziri wa nchi ofisi ya Raisi Tawala za mikoa na serikali za mitaaa (TAMISEMI) Mh Ummy Mwalimu  amesema Tsh.Trilioni 3.6  zinahitajika kwa ajili ya utekelezaji wa miradi mbalimbali ya miundombinu ya barabara nchini maeneo ya vijijini na mjini kwa kipindi cha miaka mitano.

 Waziri Ummy amebainisha hayo  Agosti 12,2021 jijini Dodoma  katika mkutano maalum wa kuweka mkakati uimarishaji wa mtandao wa barabara  vijijini na mjini  ambapo amesema katika utekelezaji wa mpango mkakati huo zaidi ya barabara za changarawe  72 elfu  zitajengwa.

“Na mnaiona kwa dhati dhamira ya Rais wetu Mpendwa Samia Suluhu Hassan kama mwaka mmoja tayari kuna bilioni 966 sioni wapi Rais Samia atashindwa kupata Tsh.Trilioni 3.6  naamini hizi Trilioni 3.6 anauwezo wa kuipata ndani ya miaka 3 na mnavyomjua Rais Samia ni ninyi wenyewe kujipanga “amesema.

Katika utekelezaji wa mpango huo waziri Ummy ametoa msisitizo kwa wakala wa barabara vijijini na mjini [TARURA]kuwa mahusiano  na baraza la madiwani pamoja na kigezo cha urefu wa barabara  kizingatiwe na kigezo cha ukubwa wa eneo husika.

“Tunapoongelea ongezeko la fedha za matengenezo na ujenzi wa barabara ni vyema kigezo cha urefu wa barabara kizingatiwe na ukubwa wa eneo husika ,umetoka Nsimbo,unatoka Mlele unatoka ,Tanganyika hakuna hata kilometa ya barabara lakini majiji yenye barabara nyingi yanaongezewa hili lazima tuliangalie upya na lazima muwe na mahusiano mema kwa kushirikisha mabaraza ya madiwani katika utekelezaji wa miradi yenu”amesema.

Aidha,Waziri Ummy ameonya kasumba ya kuleta mivutano   ya fedha kiasi cha Tsh.Mil.500 ambazo Rais Samia alitoa kila halmashauri .

“Madiwani wanagombea Mil.500 lakini uwezo wa halmashauri yao ni ukusanyaji wa Tsh.bilioni 60 nawashangaa huko Dar es Salaam Halmashauri moja ilifanya hivyo”amesema.

Msititizo mwingine ambao ameutoa Waziri Ummy kwa TARURA  ni pamoja na uandaaji wa mpango wa muda mfupi na muda mrefu  katika kuondoa vikwazo kwenye maeneo ambayo hayapitiki ,kuimarisha mahusiano ya kikazi,halmashauri kuwatumia wahandisi wa TARURA,matumizi ya teknolojia sahihi ni muhimu katika kuondoa gharama za ujenzi.

Mambo mengine ni kuandaa mpango wa usanifu wa madaraja pamoja na TARURA kutoa ushauri wa kitaalam pamoja na madiwani kuweka kipaumbele cha kusikiliza ushauri unaotolewa na TARURA.

Naye Mtendaji Mkuu wa  Wakala wa barabara vijijini na Mjini [TARURA Mhandisi Victor Seff  amesema mpango huo utakuwa na chachu kubwa katika uimarishaji wa miundombinu .
Aidha,amesema hadi kufikia Juni,30,2021 utekelezaji wa bajeti wa mwaka 2020/2021 kwa fedha za matengenezo umefikia 88% na matumizi ya fedha 72% na fedha zilizopokelewa ni 93.4%,kazi za maendeleo zikitekelezwa kwa 63%.

Kuhusu mpango wa utekelezaji wa bajeti ya mwaka wa fedha  2021/2022  mtendaji mkuu wa TARURA amesema imeharakisha taratibu za manunuzi kwa kuongeza ufuatiliaji mikoani ambapo hadi kufikia tarehe 10 Agosti 2021 mikataba 395  imekwishasainiwa  na mingine 324 inatarajiwa kusainiwa kabla ya tarehe 20,Agosti,2021 na kufanya jumla ya mikataba yote 719.

Pia,katika bajeti ya nyongeza ya Tsh.bilioni 322.128 ,zabuni 6 za miradi mikubwa imekwishatangazwa [madaraja makubwa 3  yenye urefu wa km 3327].

Mkutano Maalum wa Mkakati uimarishaji wa mtandao wa barabara  vijijini na mjini  kwa kipindi cha miaka mitano unakwenda sambamba na kauli isemayo “Tunakufungulia barabara kufika kusikofikika”


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments