Waziri wa Mambo ya Nje Balozi Mulamula Awasilisha Makadirio Ya Mapato Na Matumizi Bungeni Jijini Dodoma


Mheshimiwa Balozi Liberata Rutageruka Mulamula (Mb), Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki leo amewasilisha bungeni makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2021/2022 katika Mkutano wa Bajeti unaoendelea jijini Dodoma. 

Akiwasilisha bungeni hotuba hiyo Balozi Mulamula ameeleza kuwa ili Wizara iweze kutekeleza kikamilifu majukumu yake kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022, analiomba Bunge Tukufu liidhinishe jumla ya shilingi 192,265,438,000. Kati ya fedha hizo shilingi 178,765,438,000 ni kwa ajili ya Matumizi ya Kawaida na shilingi 13,500,000,000 ni kwa ajili ya Bajeti ya Maendeleo.

Aidha Balozi Mulamula ameyataja majukumu ambayo Wizara imeyapa kipaumbele kuyatekeleza katika Mwaka wa Fedha 2021/2022, kama ifuatavyo;

  • Kuendelea kutekeleza diplomasia ya uchumi ikiwa ni pamoja na kuwezesha balozi zetu kuwa kiungo muhimu cha kukuza uwekezaji, upatikanaji wa masoko ya bidhaa na huduma zinazozalishwa nchini na kuvutia watalii; 
  • Kuendelea kuboresha na kuimarisha uhusiano na nchi nyingine, jumuiya za kikanda na mashirika ya kimataifa;
  • Kuendelea kuweka mazingira wezeshi, kuratibu na kuhamasisha ushiriki wa Watanzania wanaoishi nje ili kushiriki kikamilifu katika kuchangia maendeleo ya nchi;
  • Kuendelea kulinda na kutetea misingi ya Taifa letu ndani na nje ya nchi;
  • Kuendelea kushawishi na kuhamasisha matumizi ya lugha ya Kiswahili kwa nchi moja moja, jumuiya za kikanda na kimataifa;
  • Kuendelea kushiriki katika juhudi za kulinda na kuimarisha amani duniani na maendeleo kupitia Umoja wa Mataifa;
  • Kuendelea kujenga na kukarabati majengo kwa ajili ya balozi zetu ili kupunguza gharama na kuleta mapato kwa Serikali;
  • Kuendelea kufungua ofisi za Balozi na Konseli Kuu mpya katika nchi za kimkakati;
  • Kuendelea kushiriki kikamilifu katika kuimarisha utangamano wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EAC) na Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC);
  • Kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu utekelezaji wa majukumu ya Wizara, masuala ya uhusiano wa kimataifa na utangamano wa kikanda; 
  • Kuendelea kusimamia utekelezaji wa majukumu ya Taasisi zilizopo chini ya Wizara; na
  • Kuendelea kusimamia rasilimali watu na fedha Makao Makuu ya Wizara na Balozini.
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania limeidhinisha bajeti ya Wizara, jumla ya shilingi 192,265,438,000 kwa Mwaka wa Fedha 2021/2022.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments