RAIS SAMIA KUFANYA ZIARA YA SIKU TATU JIJINI MWANZA

Rais Samia Suluhu anatarajiwa kuanza ziara ya kiserikali ya siku tatu mkoani Mwanza, ambapo pamoja na mambo mengine atazindua na kuweka jiwe la msingi kwenye miradi ya maendeleo ya mabilioni iliyoko mkoani Mwanza.

Akizungumza jana juu ya ziara hiyo, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, Albert Chalamila alisema ziara hiyo itaanza rasmi Juni 13 hadi Juni 15 mwaka huu, ambapo Rais atawasili jijini hapo akitokea mjini Dodoma ambapo atapata fursa ya kufungua mtambo mkubwa wa kusafisha dhahabu

Alisema mtambo huo umejengwa  katika Kiwanda cha Mwanza Precious Metal Refinery katika manispaa ya Ilemela  kwa gharama ya  kiasi Sh bilioni 10.4.

Sambamba na kiwanda hicho pia siku hiyo Rais atafungua jengo la Benki Kuu ya Tanzania (BOT)  Kanda ya Mwanza ambao ujenzi wake tayari umekamilika.

"Rais mara baada ya kuzindua jengo hilo la BOT, atapata fursa ya kuhutubia wananchi," alisema Chalamila na kuwataka wakazi wa jiji la Mwanza kujitokeza kwa wingi siku hiyo akisisitiza kuwa hii ndiyo ziara ya kwanza ya Rais mkoani Mwanza baada ya kuapishwa kuwa  Rais wa awamu ya sita kwa mujibu wa Katiba baada ya aliyekuwa Rais wa awamu ya tano John  Magufuli kufariki dunia.

Chalamila aliongeza kuwa Juni 14 Rais atakwenda wilayani Misungwi ambapo atazindua  mradi wa  maji Misungwi uliogharimu kiasi cha Sh bilioni 13.7 na kuhutubia wananchi.

"Baadaye Mheshimiwa Rais atakwenda kuweka jiwe la msingi kwenye mradi wa ujenzi wa reli ya kisasa(SGR) eneo la Fela wilayani Misungwi huo ukiwa ni ujenzi wa loti ya tano," alisema Chalamila na kumshukuru Rais Samia kutokana na kasi na dhamira aliyoionyesha kwenye mradi huo ambapo tayari serikali imeishatoa kiasi cha Sh bilioni 372 ikiwa ni malipo ya awali kwa  ajili ya ujenzi wa mradi huo.

Chalamila amefafanua kuwa Juni 15 mwaka huu, Rais Samia Suluhu Hassan atatembelea na kukagua ujenzi wa mradi wa daraja la JPM unaojengwa kwa gharama ya Sh bilioni 699 ili aweze kujionea maendeleo ya ujenzi wake.



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments