VYETI NA LESENI 246 VIMETOLEWA NA TBS KWA WAZALISHAJI WA BIDHAA NCHINI

 

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania Dkt.Athuman Yusuf Ngenya akimpatia leseni ya kutumia alama ya ubora ya uunganishaji wa mabasi Bw.Jonas Nyagawa kutoka kampuni ya BM Motors iliyopo mkoani Pwani. TBS inatoa leseni hiyo kwa mara ya kwanza Tanzania kwa Kampuni ya kitanzania inayojishughulisha na uunganishaji wa mabasi nchini.

Meneja wa Uthibitishaji ubora Bw.Gervas Kaisi akizungumza na wazalishaji waliohudhuria hafla ya utoaji leseni mapema leo, TBS Ubungo jijini Dar es salaam. Kaisi alitoa wito kwa wazalishaji hao kuhakikisha wanaendelea kuzalisha bidhaa bora wakati wote ili kuendelea kumlinda mlaji na kuunga mkono jitihada za serikali za kuendeleza Viwanda.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania Dkt.Athuman Yusuf Ngenya akimpatia leseni ya kutumia alama ya ubora mjasiriamali kutoka kampuni ya Ulanzi Halisi ya mkoani Iringa inayotengeneza pombe ya ulanzi . Mjasiriamali huyo ameishukuru TBS kwa kupata alama ya ubora na anategemea kupata soko zaidi ikiwemo nje ya nchi.

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Viwango Tanzania Dkt.Athuman Yusuf Ngenya akizungumza na wazalishaji waliohudhuria hafla ya utoaji leseni mapema leo, Makao Makuu ya TBS Ubungo jijini Dar es salaam.


NA EMMANUEL MBATILO

Shirika la Viwango Tanzania (TBS) limetoa jumla ya leseni na vyeti 246 kwa kutumia alama ya ubora wa TBS kwa wazalishaji wa bidhaa nchini.

Akizungumza katika hafla hiyo Mkurugenzi Mtendaji wa TBS, Dkt.Athuman Ngenya amesema kati ya leseni na vyeti 127 sawa na asilimia 51.63 vimetolewa kwa wajasiriamali.

"Vyeti na leseni vilivyotolewa vinahusisha bidhaa mbalimbali ikiwa ni pamoja na zile za vyakula,vipodozi,viatu,vifaa vya ujenzi, vifaa vya umeme, magodolo na vifungashio kwa pamoja". Amesema Dkt.Ngenya.

Aidha Dkt.Ngenya amesema kuwa leseni na vyeti hivyo vitasaidia bidhaa zilizothibitishwa kukubarika sokoni pamoja na kupata faida kiushindani.

Pamoja na hayo Dkt.Ngenya amesema kuwa katika kipindi cha mwezi Januari mpaka mwezi Mei mwaka huu, TBS imesajili majengo 3295 ya biashara na kuhifadhi bidhaa za vyakula na vipodozi kwa pamoja pia katika kipindi hicho wamesajili bidhaa 642 za vyakula na vipodozi kwa pamoja.

Kwa upande wake Meneja wa Uthibitishaji ubora TBS, Bw.Gervas Kaisi ametoa wito kwa wazalishaji hao kuhakikisha wanaendelea kuzalisha bidhaa bora wakati wote ili kuendelea kumlinda mlaji na kuunga mkono jitihada za serikali za kuendeleza Viwanda.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments